Singapore mji ghali zaidi duniani
Singapore umetajwa kuwa mji ghali zaidi duniani kuishi kwa mwaka 2014 na
kuipiku miji mingine 131 kwa mujibu wa taarifa ya Economist
Intelligence Unit (EIU).
Nguvu ya sarafu ya mji huo ikiwa ni pamoja na gharama kubwa ya
uendeshaji magari na kuongezeka kwa malipo ya huduma za umma kumechangia
Singapore kuwa juu ya miji yote duniani kwa ughali wa maisha.
Pia ni mahali ambapo nguo zinauzwa kwa bei ya juu kabisa kuliko miji yote duniani.
Singapore imechukua nafasi ya mji wa Tokyo, amao ulikuwa unaongoza kwa ughali wa maisha mwaka 2013.
Miji mingine mitano inayoongoza kwa gharama
kubwa za maisha duniani ni pamoja na Paris, Oslo, Zurich na Sydney, huku
Tokyo ukiporomoka hadi nafasi ya sita.
Mji wa New York unatumiwa kama kigezo cha
utafiti wa shirika la EIU kuhusu gharama za maisha katika miji
mbalimbali duniani. Wanaangalia zaidi ya bei binafsi 400.
Magari ya umma yavuruga shughuli Nairobi
Huduma za usafiri jijini Nairobi zimekwama kufuatia hatua za wenye
magari kugoma hii leo wakilalamikia nyongeza ya ada ya kuegesha magari
jijini humo
. Mgomo wa wahudumu wa magari nchini Kenya
Maelfu ya wafanyakazi wamelazimika kutembea kwa miguu na wasafiri wa
kutoka jijini kwenda maeneo ya mashambani nao kulazimika kuahirisha
safari zao.
Mwenyekiti
wa wenye matatu katika eneo la Mlima Kenya, Bwana Michael Kariuki,
ambaye aliongea na BBC akiwa nje ya lango la kuingia kwenye afisi ya
Gavana wa Kaunti ya Nairobi, alisema mzozo uliopo ni mdogo na waweza
kusuluhishwa haraka.
"Juzi tulikuwa na Gavana Evans Kidero na
tukakubaliana kiasi tunachopaswa kulipa lakini jana tulipofika
wafanyakazi wa kaunti wakakataa kiasi tulichokuwa nacho," Bwana Kariuki
alisema.
Jiji la Nairobi ni mojawapo wa kaunti ambazo
zimebuniwa chini ya Katiba iliyopitishwa na wapiga kura na kuidhinishwa
mwaka 2010 katika hatua ya kuimarisha huduma kwa wananchi.
Kaunti hizo mpya hata hivyo zimejikuta njia
panda baada ya kupata madaraka bila fedha za kuandamana nayo; ambapo
zimelazimika kuongeza kodi kama njia mojawapo ya kujiimarisha kiuchumi.