Monday 24 March 2014

Zanzibar yashauriwa kurekebisha Katiba

 

 Alisema wakati Katiba ya Zanzibar ikieleza hivyo, Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania sura ya 1 inaelezaa kuwa Tanzania ni nchi moja na eneo lake la mipaka ni kuanzia Tanzania Bara hadi Visiwani

Zanzibar. Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) imeshauriwa kufanya marekebisho ya Katiba kabla ya Uchaguzi Mkuu Mwaka 2015 ili kuondoa vifungu vinavyogongana na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Ushauri huo umetolewa na mwanasiasa mkongwe wa Zanzibar, Ali Hassan Khamis wakati akiwasilisha mada juu ya hali ya kisiasa na mchakato wa Katiba ya Muungano katika kongamano lililoandaliwa na Jumuiya za CCM, lililofanyika kwenye Ukumbi wa Tawi la Kiembesamaki Mkoa wa Mjini Magharibi Unguja.
Alisema migongano inayojitokeza katika Muungano wa Tanganyika na Zanzibar imetokana na marekebisho ya 10 ya Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 iliyogongana na Katiba ya Muungano na kusababisha mjadala mkubwa katika mchakato wa mabadiliko ya katiba unaoendelea.
Alisema marekebisho hayo ya Katiba ya Zanzibar yameongeza migongano hasa sura ya 1(1) inayoeleza kuwa Zanzibar ni nchi ambayo eneo la mipaka yake ni eneo lote la Visiwa vya Unguja na Pemba pamoja na visiwa vidogo vilivyozungukwa na bahari yake, ambayo kabla ya Muungano wa Tangayika na Zanzibar ilikuwa ikiitwa Jamhuri ya Watu wa Zanzibar.
Alisema wakati Katiba ya Zanzibar ikieleza hivyo, Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania sura ya 1 inaelezaa kuwa Tanzania ni nchi moja na eneo lake la mipaka ni kuanzia Tanzania Bara hadi Visiwani.
Aliwaeleza washiriki hao kuwa kifungu cha 2(a) cha Katiba ya Zanzibar kimempa uwezo Rais wa Zanzibar kuigawa Zanzibar katika mikoa na wilaya kinyume na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977.
Alisema marekebisho hayo ya 10 yamechangia kwa kiwango kikubwa kuibua migogoro ndani ya Muungano na kutaka Katiba ya Zanzibar iandikwe upya na wananchi wapewe nafasi ya kuijadili na kuamua.
Muungano wa Tanganyika na Zanzibar.
Vilevile alieleza katika marekebisho hayo ya 10 kuna vitu viliondolewa lakini havikuwa na ulazima kama wakuu wa mikoa kuwa wajumbe wa Baraza la Wawakilishi (BLW), wakati ni watendaji wakuu wa shughuli za Serikali katika kuwahudumia wananchi kwenye maeneo yao.
“Wakati umefika katiba yetu ya Zanzibar iangaliwe upya iendane na Katiba ya Jamhuri ya Muungano vinginevyo tutaendelea kuendeleza migogoro na kuathiri msingi mzima wa Muungano na Mapinduzi ya Zanzibar,” alisema Ali Hassan Mkuu wa Wilaya ya Kati wa zamani visiwani humo.
Akifafanua zaidi alisema hata muundo wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa (SUK), una kasoro Zanzibar kutokana na sera ya CCM kuwa ni moja kati ya Zanzibar na Tanzania Bara lakini mfumo huo wa Serikali umezingatiwa upande marekebisho hayo ya kati mmoja wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
“Chama chetu ni kimoja, ni sehemu gani sera yetu imesema CCM ikishinda itaunda Serikali ya Umoja wa Kitaifa wakati hilo Tanzania Bara halipo,” alisema.

 

Ikulu: Kujadili hotuba ya JK kupoteza muda

Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais Ikulu, Salva Rweyemamu

Dar es Salaam. Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais Ikulu, Salva Rweyemamu amesema kuendelea kuijadili hotuba ya Rais Jakaya Kikwete aliyotoa kwenye Bunge la Katiba mwishoni mwa wiki ni kupoteza muda.
Akizungumza na gazeti hili jana, Rweyemamu aliushangaa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) kuendelea kutoa matamko yanayoipinga hotuba hiyo, akisema haumtendei haki mkuu huyo wa nchi na Watanzania wote kwa ujumla. Alisema kama Mtanzania, Rais alitoa maoni yake na amekuwa muungwana kwa kuwaambia kwamba bado wana fursa ya kujadili na kuleta mapendekezo yao, lakini wajali zaidi masilahi ya taifa.
“Hiyo ni propaganda isiyokuwa na maana kwa taifa na hata hatima ya Katiba yenyewe. Ningependa kuwakumbusha kwamba Watanzania wamewapeleka Dodoma wakajadili Katiba na siyo kufanya propaganda, tunawataka wafanye kazi,” alisema Rweyemamu.
Kwa mujibu wa Rweyemamu, umoja huo wenye viongozi kutoka vyama vya upinzani haumtendei haki Rais kwani kama Mtanzania, mkuu huyo wa nchi ana fursa ya kutoa maoni yake.
“Wasifikiri kwa kumjibu hivyo Rais wanajibizana na CCM. Rais ni mkuu wa nchi ana maoni yake, lakini zaidi ya yote, Bunge la Katiba siyo mahali pa kufanya siasa. Kama wanataka siasa tunawaomba warudi maofisini mwao wakafanye siasa, pale tumewatuma kazi,” alisisitiza.
Rweyemamu alibainisha kuwa mchakato wa kutunga Katiba unahitaji busara na busara hiyo haiwezi kupatikana kama watu waliotumwa kuwawakilisha wananchi wameamua kufanya siasa.
“Tunahitaji watu wote wawe CCM, CUF, Chadema na vyama vingine waache siasa,” alisema.
Wakati huohuo, bungeni Dodoma limeibuka kundi la wajumbe, wengi wao kutoka CCM wakiipongeza hotuba hiyo ya Rais Jakaya Kikwete na kuwakosoa watu wanaotishia kumpeleka Rais mahakamani kwa madai ya kuvunja kanuni na Sheria ya Mabadiliko ya Katiba kwa kuingilia mchakato wa maoni.
Mjumbe wa kundi hilo linalojiita Tanzania Kwanza, Evod Mmanda alisema siyo kweli kuwa Rais amevunja sheria kwani alihutubia Bunge baada ya kupitishwa kwenye kanuni za Bunge kifungu cha 75(1) ambacho kinaeleza mwenyekiti anaweza kumwalika mgeni rasmi kulihutubia Bunge.
Walioambatana na Mmanda ni Dk Emmanuel Nchimbi, Said Nkumba, Mohamed Thabit Kombo, Waride Jabu, Seleman Jafo na Charles Mwijage.

Bunge la Katiba Njiapanda

“Kama tunataka serikali ya tatu lazima tuitengenezee misingi ya uhakika na kuhoji nani atayeidhamini serikali ya tatu virungu, pingu, magari ya kuwasha, majeshi au bunduki.”
Dar es Salaam. Kwa neno moja unaweza kusema kwamba wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba na wananchi kwa ujumla wako “njiapanda”.
Hii ni baada ya hotuba ya ufunguzi wa Bunge hilo iliyotolewa na Rais Jakaya Kikwete kuibua mambo mazito ambayo kimsingi yanatofautiana na mapendekezo yaliyomo katika Rasimu ya Katiba iliyowasilishwa bungeni na mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba.
Huku wananchi wakijiuliza nini hatima ya Bunge hilo baada ya hotuba hiyo, baadhi ya wajumbe ambao wiki hii ndiyo wanaanza kujadili rasimu hiyo, watakuwa katika wakati mgumu wa kuamua wafuate maoni ya nani, kati ya viongozi hao wawili.
Ingawa Rais Kikwete amesema mara kadhaa kuwa wajumbe wa Bunge la Katiba ndiyo waamuzi. Mambo mengi aliyoibua yanaonyesha kutokubaliana kwake na baadhi ya maoni ya wananchi yaliyomo katika rasimu, ambayo Jaji Warioba amewahi kusema kuwa yanatakiwa kuheshimiwa.
Wakizungumzia tofauti hizo, mjumbe wa Bunge la Katiba, Ezekiah Oluoch alisema kauli za Rais Kikwete na Jaji Warioba zimezidi kuwagawa wajumbe wa Bunge hilo kwa maelezo kuwa tangu awali wajumbe hao walikuwa wamegawanyika katika makundi mawili; ya wanaotaka muundo wa Muungano uwe wa serikali tatu na wale wanaotaka serikali mbili.
Alisema kama suala la muundo wa Serikali likishindikana kupatiwa mwafaka ni vyema likarudishwa kwa wananchi ili wapige kura ya maoni kuchagua aina wanayoitaka, kisha suala hilo lirejeshwe tena katika Bunge la Katiba kwa ajili ya kuboreshwa.
“Rais alipoanza kuzungumza alikuwa kama mkuu wa nchi lakini mwisho wa hotuba yake aligeuka kuwa mwenyekiti wa CCM. Kifupi alichokizungumza kimekwenda tofauti na wadhifa wake,” alisema.
Naye Deo Filikunjombe alisema: “Nadhani kwa hotuba hizi mbili, kazi ya wajumbe wa Bunge la Katiba itakuwa rahisi. Maana sasa wameshajua uzuri na ubaya wa serikali tatu na mbili.
“Hata kama kutakuwa na tofauti, wananchi ndiyo watakuwa wa mwisho kuamua kama Katiba hii ipite au isipite. Tunachotakiwa wajumbe ni kuwa makini na uamuzi wetu.”
Naye Yusuf Manyanga alisema: “Bunge la Katiba limejaa watu wenye busara. Sidhani kama tutashindwa kuelewana maana hata katika biashara ya utumbo inzi ni wengi lakini utumbo unauzika.”
Katika hotuba yake aliyoitoa Ijumaa iliyopita Rais Kikwete aligusia mambo saba ya msingi yaliyomo katika rasimu ya Katiba na kutaka yatazamwe kwa kina, huku akibainisha kuwa mengine hayawezekani kutekelezeka.

 

Sitta ‘amkataa’ Warioba bungeni

Mwenyekiti wa Bunge maalumu la katiba, Samuel Sitta 

Dodoma. Jaribio la kutaka kumrejesha bungeni Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba ili ajibu masuala yaliyoibuliwa na Rais Jakaya Kikwete katika hotuba yake ya kufungua Bunge limegonga mwamba.
Uamuzi wa kukataa ombi hilo ulitolewa jana na Mwenyekiti wa Bunge hilo, Samuel Sitta wakati akijibu mwongozo ulioombwa na Mjumbe wa Bunge, Julius Mtatiro, akisema hadhani kama ni sahihi ombi hilo kutekelezwa.
Awali Mtatiro aliomba mwongozo kwa mwenyekiti, akitaka kujua iwapo kuna haja ya kumrejesha Jaji Warioba kutoa ufafanuzi juu ya baadhi ya hoja za Rais Kikwete ambazo zimekinzana na maoni ya wananchi yaliyomo kwenye Rasimu ya Katiba.
Mtatiro alisema: “Mtoa hoja mahususi alikuwa ni Jaji Warioba na Rais Kikwete alialikwa kama mgeni rasmi kufungua Bunge, lakini badala yake alikuja kujibu hotuba ya Warioba.
“Kwa sababu Rais alikaribishwa kama mgeni rasmi, lakini  alijibu  hoja za Warioba, je, hatuoni kama kuna haja ya kumrejesha mtoa hoja mahususi aje kujenga hoja  kutokana na alichosema Rais Kikwete?” alihoji Mtatiro ambaye pia ni Naibu Katibu Mkuu wa CUF.
Katika ufafanuzi wake, Sitta alisema tayari amepokea kwa maandishi kutoka kwa baadhi ya wajumbe kuzungumzia suala hilo, jambo ambalo litafanyika lakini si kwa kumwita tena Jaji Warioba. Tunapenda kupata muda wa kuzungumzia  suala hili ili kuliweka sawa, hotuba zote mbili ambazo ni muhimu zitaandaliwa ili kupitiwa kuona kama malalamiko yanayotolewa yana hoja,” alisema Sitta.
Tangu Rais Kikwete ahutubie Bunge Ijumaa na kutoa hoja kinyume na mapendekezo ya Rasimu ya Katiba, hasa muundo wa Muungano, kumeibuka mijadala ya ama kuipinga au kuiunga mkono, huku wengine wakieleza kuwa imekiuka sheria.

 

 

 

Marekani kusaidia UG kupambana na Kony


Kiongozi wa waasi wa LRA Joseph Kony

 Serikali ya Marekani inatuma ndege ya kivita na kikosii maalum cha jeshi kusaidia Uganda katika juhudi za kumsaka kiongozi wa kundi la waasi la Lord's Resistance Army, Joseph Kony.Msemaji wa baraza la usalama la Marekani, Caitlin Hayden, amesema kuwa wanajeshi wa Afrika wataendelea kuongoza operesheni hiyo, ingawa watapata ushauri kutoka kwa vikosi vya Marekani.Alisema kuwa ndege hiyo itawekwa nchini Uganda ingawa itatumika katika nchi zingine ambako waasi wa LRA wamekuwa wakijificha.Marekani ilituma vikosi vyake mara ya kwanza nchini Uganda mwaka 2011 kusaidia Uganda katika harakati za kumtafuta Joseph Kony.

 

529 wahukumiwa kifo Misri

Mahakama nchini Misri imewahukumu kifo watu 529 ambao wanasemekana kuwa wafuasi wa Rais aliyeng'olewa mamlakani Mohammed Morsi.
Watu hao walikabiliwa ma mashitika mbali mbali yakiwemo mauaji ya polisi na kuwavamia polisi.
Wafuasi hao wa chama kilichopigwa marufuku, cha Muslim Brotherhood, ni sehemu ya kundi lengine kubwa la watu zaidi ya 1,200 wanaoaminika kuwa wafuasi wa Morsi.
Maafisa wa utawala nchini Misri wamekuwa wakiendesha msako mkubwa dhidi ya wafuasi wa vuguvugu hilo, tangu Morsi kuondolewa mamlakani mwezi Julai mwaka jana.
Maelfu wamekamatwa huku mamia wakiuawa.
Mahakama hiyo ilitoa hukumu baada ya vikao viwili pekee ambapo mawakili wa watuhumiwa walilalamika kuwa hawakupewa muda wa kuwasilisha kesi yao vyema.
Mauaji wanayodaiwa kufanywa na watuhumiwa yalitokea Kusini mwa Misri, mwezi Agosti, baada ya vikosi vya usalama kuvunja kambi mbili za wafuasi wa Morsi waliokuwa wanataka arejeshwe mamlakani

 

Makahaba watumia Vibaya Hijab Kenya

Makahaba katika baadhi ya sehemu za mji mkuu wa Kenya , Nairobi, wametupilia Mbali vazi la 'Mini skirt na kuanza kutumia Hijab kama njia ya kuwavutia wateja wao, jambo ambalo limekashifiwa vikali na wakuu wa dini ya Kiislamu.
Hijab huvaliwa na wanawake wa Kiislamu kama ishara ya kumcha Mungu, lakini makahaba katika mtaa wa Eastleigh, viungani mwa Nairobi wanatumia Hijab ili kuwafanya wateja wao kudhania kua wanatoka sehemu za Pwani.
Taarifa hii ni kwa mujibu wa mtandao wa shirika la habari la Nation mjini Nairobi.
Mwanamke mmoja ambaye hakutaka kutaja jina lake alisema kuwa yeye hupata wateja maradufu kwani huvalia vazi hilo la Hijab, wengi wa wateja wake wakimuona kama mwenye nidhamu.
Uchunguzi ulibaini kuwa wanawake wasio wa kiislamu wanavalia vazi hilo ili kuwavutia wanaume ambao wanaamini kuwa wao wana maadili zaidi ya wale wanaovalia nguo fupi au 'Mini Skirt'.
Nguo fupi ni mavazi yaliyozoeleka kwa makahaba sehemu nyingi duniani
Taarifa hiyo imemnukuu Imam mkuu wa msikiti wa Jamia mjini Nairobi, Mohamed Swalihu akisema kuwa ni jambo la kusikitisha sana kuwa Hijab inatumika kwa njia isiyopaswa na makahaba huku akiongeza kuwa pia wanaume wanalitumia vazi hilo kuendesha shughuli za uhalifu jambo ambalo amelitaja kuwa la kishetani linalostahili kukashifiwa vikali.
Hata hivyo chama cha makahaba nchini Kenya kimewatetea makahaba hao wanaotumia hijab huku likidai kwamba wanafanya hivyo ili kukidhi mahitaji ya wateja wao.
Mratibu wa muungano huo, Bi Phelister Abdalla, aliiomba serikali kuhalalisha ukahaba kwa madai ya viwango vya juu vya ukosefu wa ajira.
Mahojiano na makahaba katika mtaa wa Eastleigh yalibaini kwamba wanaume hawakuwa na haja ya wanawake wenye kuvalia nguo fupi badala yake wakipendelea wanawake wa kiislamu na wale wa kutoka Ethiopia.