Bunge la Katiba Njiapanda
“Kama tunataka serikali ya tatu lazima tuitengenezee misingi ya uhakika
na kuhoji nani atayeidhamini serikali ya tatu virungu, pingu, magari ya
kuwasha, majeshi au bunduki.”
Dar es Salaam. Kwa neno moja unaweza kusema kwamba wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba na wananchi kwa ujumla wako “njiapanda”.
Hii ni baada ya hotuba ya ufunguzi wa Bunge hilo
iliyotolewa na Rais Jakaya Kikwete kuibua mambo mazito ambayo kimsingi
yanatofautiana na mapendekezo yaliyomo katika Rasimu ya Katiba
iliyowasilishwa bungeni na mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba,
Jaji Joseph Warioba.
Huku wananchi wakijiuliza nini hatima ya Bunge
hilo baada ya hotuba hiyo, baadhi ya wajumbe ambao wiki hii ndiyo
wanaanza kujadili rasimu hiyo, watakuwa katika wakati mgumu wa kuamua
wafuate maoni ya nani, kati ya viongozi hao wawili.
Ingawa Rais Kikwete amesema mara kadhaa kuwa
wajumbe wa Bunge la Katiba ndiyo waamuzi. Mambo mengi aliyoibua
yanaonyesha kutokubaliana kwake na baadhi ya maoni ya wananchi yaliyomo
katika rasimu, ambayo Jaji Warioba amewahi kusema kuwa yanatakiwa
kuheshimiwa.
Wakizungumzia tofauti hizo, mjumbe wa Bunge la
Katiba, Ezekiah Oluoch alisema kauli za Rais Kikwete na Jaji Warioba
zimezidi kuwagawa wajumbe wa Bunge hilo kwa maelezo kuwa tangu awali
wajumbe hao walikuwa wamegawanyika katika makundi mawili; ya wanaotaka
muundo wa Muungano uwe wa serikali tatu na wale wanaotaka serikali
mbili.
Alisema kama suala la muundo wa Serikali
likishindikana kupatiwa mwafaka ni vyema likarudishwa kwa wananchi ili
wapige kura ya maoni kuchagua aina wanayoitaka, kisha suala hilo
lirejeshwe tena katika Bunge la Katiba kwa ajili ya kuboreshwa.
“Rais alipoanza kuzungumza alikuwa kama mkuu wa
nchi lakini mwisho wa hotuba yake aligeuka kuwa mwenyekiti wa CCM.
Kifupi alichokizungumza kimekwenda tofauti na wadhifa wake,” alisema.
Naye Deo Filikunjombe alisema: “Nadhani kwa hotuba
hizi mbili, kazi ya wajumbe wa Bunge la Katiba itakuwa rahisi. Maana
sasa wameshajua uzuri na ubaya wa serikali tatu na mbili.
“Hata kama kutakuwa na tofauti, wananchi ndiyo
watakuwa wa mwisho kuamua kama Katiba hii ipite au isipite.
Tunachotakiwa wajumbe ni kuwa makini na uamuzi wetu.”
Naye Yusuf Manyanga alisema: “Bunge la Katiba
limejaa watu wenye busara. Sidhani kama tutashindwa kuelewana maana hata
katika biashara ya utumbo inzi ni wengi lakini utumbo unauzika.”
Katika hotuba yake aliyoitoa Ijumaa iliyopita Rais
Kikwete aligusia mambo saba ya msingi yaliyomo katika rasimu ya Katiba
na kutaka yatazamwe kwa kina, huku akibainisha kuwa mengine hayawezekani
kutekelezeka.
No comments:
Post a Comment