Friday, 7 March 2014
Obama awasiliana na Putin kuhusu Ukraine
Mawasiliano kati ya Putin na Obama.
Rais Obama amefanya mazungumzo
zaidi ya kina na rais wa Urusi Vladmir Putin akisistiza kuwa vitendo vya
nchi yake katika jimbo la Crimea ni ukiukaji wa mipaka na uhuru wa
taifa la Ukraine.
Wakati wa mazungumzo yao ya pili kupitia njia ya
simu katika kipindi cha siku sita zilizopita, bwana Obama amependekeza
njia ya kusuluhisha mzozo huo kidiplomasia inayojumuisha Urusi kuwaondoa
wanajeshi wake katika jimbo la Crimea. Bwana Putin amesema uhusiano
kati ya Moscow na Washington haufai kutatizika kutokana na mzozo wa
Ukraine.Awali bwana alisema kuwa kura ya maoni iliyopendekezwa kuhusu jimbo la Crimea kujiunga na Moscow inakiuka sheria ya kimataifa na sharti ijumuishe serikali ya Kiev iwapo itaandaliwa.
Akizungumza baada ya mkutano mwingine wa Baraza la Usalama uliofanyika faraghani, balozi wa Uingireza katika umoja wa mataifa , Mark Lyall Grant, amesema haiwezekani muafaka kupatikana katika baraza hilo kuhusu mzozo huo.
Bunge la Crimea limepiga kura kujitenga na Urusi.
''Pengine kiwango fulani cha makubaliano kitaafikiwa ili kutuliza mgogoro huu na kisha baraza la usalama pengine litapata suluhu. Lakini hatujafutilia mbali mpango wa kuwasilisha azimio mbele ya Baraza la Usalama wakati wowote na tunafuatilia hali ya mambo kwa karibu tukitarajia baraza la Usalama likutane tena katika siku chache zijazo ikitegemea kitakachotokea mashinani."
Mzozo huo wa Ukraine umechochea wanasiasa pamoja na wageni wengine mashuhuri kususia mashindano ya Olimpiki ya wanariadha walemavu nchini Urusi. Marekani imeondoa ujumbe wake katika michezo hiyo na mawaziri wa Uingereza hawatakuwepo sawia na wenzao kutoka mataifa mengine ya Ulaya.
Wanadiplomasia watimuliwa Venezuela
Serikali ya Venezuela imemtimua Balozi wa Panama na wanadiplomasia wengine wakati huu kukiwa na maandamano ya upinzani nchini humo.
Maafisa hao walipewa saa 48 kuondoka nchini Venezuela.
Takriban watu 20 wameuawa wakati wa maandamano ya kuipinga serikali ya Venezuela mwezi uliopita.
Maduro ameishutumu Panama kupanga njama za kuiangusha serikali yake.
Raia wa Venezuela kwa muda mrefu wamekua wakilalamikia ongezeko la vitendo vya uhalifu, kupanda kwa gharama za maisha na ukosefu wa bidhaa muhimu.
Sasa malaria yakwea milima.
Kimelea kinachosababisha Malaria. Mbu hawapendi mazingira ya baridi.
Watafiti kutoka Uingereza na
Marekani wanasema kuwa mabadiliko ya hali ya hewa huenda yakazua
ongezeko kubwa la maambukizi ya ugonjwa wa Malaria kote duniani huku
ugonjwa huo ukienea katika maeneo ya milimani barani Afrika na Amerika
ya Kusini.
Katika matokeo ya utafiti yaliyochapishwa kwenye
jarida la Science, wanasayansi hao wanasema hata ongezeko dogo katika
viwango vya joto siku za usoni huenda likaongeza kwa mamilioni
maambukizi ya malaria.
Mbu anayesababisha malaria.
Watu wanaoishi katika maeneo ya nyanda za juu wanakosa kinga na hivyo kurahisisha maradhi ya malaria kuenea.
Takriban watu milioni mia mbili ishirini kote duniani huambukizwa ukonjwa wa malaria.
Mnyika atishia kuwataja vigogo
Wakati
huohuo, Waziri Kivuli wa Nishati na Madini, John Mnyika ametishia
kuwataja kwa majina vigogo wa Serikali na CCM aliosema wako nyuma ya
‘kashfa’ kuhusu mgogoro huo ili waweze kuhojiwa kwa umma iwapo Waziri wa
Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo hatajitokeza kufafanua
kauli alizozitoa bungeni kutuhumu IPTL.
Mnyika ambaye pia ni Mbunge wa Ubungo (Chadema),
alisema hayo katika taarifa yake kwa vyombo vya habari, akimtuhumu
Waziri Muhongo kwa kudai bungeni Mei 25, 2013 kuwa yeye hakutumwa
wizarani kupekua mafaili ili kufuatilia mlolongo wa kesi za IPTL.
Alisema anachukua hatua hiyo kwa kuzingatia kwamba
madaraka na mamlaka ni ya wananchi... “Serikali inafanya kazi kwa niaba
ya wananchi; hivyo pale Serikali inapochelewa kuchukua hatua kutokana
na udhaifu, uzembe, ufisadi au uongo, ni muhimu wananchi wakashiriki
kutaka uwajibikaji.”
Wavuvi: Mradi wa gesi unatupunguzia samaki baharini
Katika kipindi cha zaidi ya miaka miwili sasa upatikanaji wa
samaki wa kitoweo katika pwani ya Bahari ya Hindi, eneo la Mkoa wa
Mtwara, umekuwa mgumu.
Uchunguzi uliofanywa na mwandishi wa makala haya
hivi karibuni, umebaini kuwa mabadiliko ya hali ya hewa na zana duni za
uvuvi zinachangia hali hiyo.
Lakini wakazi wa Mtwara ambao baadhi yao
wanategemea uvuvi, wanaamini kuwa upungufu wa samaki, umechangiwa na
ongezeko kubwa la mahitaji ya samaki tofauti na uwezo wa wavuvi
kulilisha soko la walaji.
Pamoja na wavuvi kukiri kuongezeka kwa soko la
samaki, wanasema upatikanaji wake umekuwa mgumu hata kwa wale
wanaotumia zana nzuri katika uvuvi.
Wavuvi wanaamini kuwa uchimbaji wa nishati ya gesi
asilia imesababisha mabadiliko ya hali ya hewa baharini kutokana na
matumizi ya kemikali za kulipua ndani ya bahari wakati wa utafiti na
uchimbaji.
“Hapo awali kabla ya kuanza uchimbaji wa gesi
asilia baharini, tulikuwa na upepo wa matalai, upepo wa mlaji na upepo
wa umande. Pepo hizo zilikuwa mwongozo kwetu kwenye shughuli zetu za
uvuvi,” anasema Ali Hamis Kimbaumbau, mvuvi na mkazi wa mjini Mtwara.
Anafafanua kuwa pepo za matalai na umande ambazo
ni upepo wa kusini huwa ni shwari na zikiambatana na upepo ambao ulikuwa
unatoa fursa kwa wavuvi wanaotumia mitumbwi kwenda baharini. Kipindi
hicho wavuvi walikuwa wanapata samaki ingawa si kwa kiwango kikubwa.
Anabainisha kuwa kwa sasa pepo wanazopata ni za
kaskazi ambazo huambatana na upepo mkali, hali inayozuia wavuvi wenye
mitumbwi isiyotumia mashine kushindwa kwenda baharini. Wavuvi
wanaofanikiwa kwenda baharini hurudi na mapato duni.
Mvuvi mwingine, Salumu Liwanje (36) anasema
wamefikia hatua ya kuamini utafiti na uchimbaji wa gesi asilia baharini
ndiyo chanzo.
Anaeleza kuwa siku moja wakiwa baharini, eneo la
Luvula walibaini nyaya zenye umeme baharini na walirushwa wakati
walipojaribu kugusa maji hayo. Alisema baadaye walisikia sauti ya
milipuko mara kadhaa hali waliyodai inaharibu mazingira ya asili ya
bahari.
“Joto limeongezeka sana baharini. Hiyo hali si ya
kawaida, ukiingia bahari kuu utakutana na joto ambalo si la kawaida
kabisa. Sisi tulizoea nyakati za usiku baharini kunakuwa na baridi kali,
lakini hali ni kinyume kwa sasa,” anabainisha Liwanje.
“Unajua wengine tukisema mabadiliko tunayoyaona
wapo, watakaosema ni walewale wasiopenda mradi wa gesi. Sasa sisi kama
wavuvi tukigusa yale maji yaliyotandazwa nyaya tunarushwa na umeme, je
samaki wataishi eneo hilo? ” anahoji mvuvi huyo.
Wafanyakazi Muhimbili walilia Sh800 mil zao
Dar es Salaam. Wafanyakazi wa Hospitali ya
Taifa ya Muhimbili (MNH) wameulalamikia uongozi wa hospitali hiyo kwa
kushindwa kuwalipa fedha zao na kuzitumia kinyume na utaratibu
uliopangwa.
Fedha zinazotajwa kutolipwa ni pamoja na Sh800
milioni za posho ya awamu ya tatu zinazotokana na mapato ya wateja wa
Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya ambazo imedaiwa zilitumika kununulia
vifaa tiba vya hospitali hiyo na fedha za likizo za tangu mwaka jana.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti wafanyakazi hao
walisema hawajalipwa posho hizo tangu Januari, 2013 baada ya kuelezwa na
mkurugenzi wa hospitali hiyo kuwa fedha hizo zitaelekezwa kununulia
vifaa vya hospitali.
“Tunashindwa kuelewa hawa viongozi wetu! wanatumia
fedha kwa maelekezo tofauti, hii inasababisha kuwapo na migogoro ndani
ya kazi,” alisema mmoja wa wafanyakazi hao.
Mtoa habari huyo alisema wafanyakazi wameshangazwa
na kauli ya Mkurugenzi Mkuu wa hospitali hiyo, Dk. Marina Njelekela
kudai hawatalipwa posho na kwamba fedha hizo zitanunulia vifaa.
“Tunatakiwa kulipwa fedha hizo kama tahadhari.
Mfano unaweza ukamuhudumia mgonjwa wa Ukimwi na ikatokea katika kumtibia
akakuambukiza hela hii unayolipwa ndiyo kazi yake,” alisema.
Ofisa Uhusiano Mwandamizi wa hospitali hiyo, Aminiel Aligaesha alikiri uongozi wa MNH kutumia fedha hizo kwa matumizi mengine.
Waziri wa Afya na Ustawi wa jamii, Dk. Seif Rashid
alisema alipata taarifa hizo na walikaa kikao na Bodi, mkurugenzi na
chama cha Tughe kujadiliana suala hilo kwa kuwa ni la kisheria zaidi.
“Hili suala lipo kisheria zaidi. Niliwaagiza
waende wakakae pamoja wajadiliane waweze kupata mwafaka ili wawalipe
wafanyakazi hao,” Dk. Seif.
Ngumi mkononi bungeni
Mjumbe wa Bunge Maalumu la Katiba, Magdalena Sakaya (kushoto), akizozana
na Magdalena Likwina baada ya Semina ya Kupitia Vifungu vya Rasimu ya
Kanuni kuahirishwa kutokana na vurugu zilizotokea bungeni jana. Picha na
Silvan Kiwale
Dodoma. Ngumi mkononi ndilo neno jepesi ambalo
linafaa kutumika baada ya vurugu kubwa kutokea jana ndani ya Ukumbi wa
Bunge Maalumu la Katiba kiasi cha kumlazimisha Mwenyekiti wa Muda, Pandu
Ameir Kificho kuahirisha semina kabla ya wakati wake.
Semina ya wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba,
imekuwa ikianza saa 4:00 asubuhi hadi saa 7:00 mchana kabla ya kuendelea
tena kuanzia saa 11:00 jioni hadi saa 3:00 usiku. Jana, katika kipindi
cha asubuhi, semina hiyo iliahirishwa saa 6:17 licha ya kuanza saa tano
asubuhi kabla ya kurejea tena saa 10 jioni.
Ngumi zilitaka kupigwa baada ya Waziri wa Katiba
na Sheria wa Zanzibar, Abubakari Hamis Bakari kuhoji uhalali wa
Christopher Ole Sendeka na Ummy Mwalimu kuchangia wakati hawakuwamo
katika orodha ya wachangiaji jambo ambalo liliibua mjadala mkali na
kurushiana maneno kabla ya Mwenyekiti Pandu Ameir Kificho kuahirisha
semina hiyo.
Chanzo cha vurugu
Kificho alimpa Ole Sendeka nafasi ya kuchangia
Kifungu namba 58 cha rasimu ya kanuni na baada ya kutoa mchango wake,
Hamisi ambaye pia ni Mjumbe wa Kamati ya Kanuni, alisimama na kumtaka
Mwenyekiti Kificho kuacha kuwateua watu ambao hawamo katika orodha ya
wachangiaji.
Kificho hakumsikiliza na badala yake, alimpa
nafasi mjumbe mwingine wa Bunge hilo Ummy Mwalimu ambaye pia ni Naibu
Waziri, Ofisi ya Makamu wa Rais, kuchangia. Hata hivyo kabla hajafanya
hivyo, Bakari alisimama tena na kumzuia kuchangia kwa madai kuwa
hakuwamo kwenye orodha ya wachangiaji.
“Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tutaendelea na
utaratibu huu suala la kuchangia kanuni linaweza kutupeleka hadi miezi
sita bila ya kumaliza. Haya majina hayakuwemo kwenye orodha ya
wachangiaji na huyo aliyemaliza sasa Ole Sendeka, naye hakuwamo, naomba
tuache mchezo huu,” alisema Bakari.
Aliendelea: “Sekretarieti inakuchomekea majina
mwenyekiti na kama hivyo ndivyo, basi tunatakiwa kuwachukulia hatua kali
hawa kwani tunataka kujadili hoja ambazo hazimo.”
Bakari alisema wajumbe waliotakiwa kuchangia ni
wale ambao walipeleka majina kwa makatibu wa Bunge hilo pamoja na
michango yao kwa maandishi ili wapewe nafasi ya kuzungumza, lakini
Kificho alikuwa akiwateua wajumbe ambao hawamo katika orodha hiyo.
Kificho ajibu
“Mimi sina tatizo na jambo hilo, mkisema tuendelee
basi sawa, lakini mkitaka tufanye mambo kwa uzuri inawezekana pia,
jambo la muhimu ni kuwa tupo hapa kutengeneza Katiba ya wananchi siyo ya
vyama.”
Kelele zilianza kusikika huku wajumbe wakiimba
kuwa mwenyekiti anayumba… na kumtaka mwenyekiti atoke nje na kukiacha
kiti, kwani anafanya upendeleo.
Suleiman Abdallah: Mwanafunzi wa IFM aliyechora nembo ya ukumbi wa Julius Nyerere
Abdallah anayechukua shahada ya Mawasiliano ya Habari na Teknolojia
(ICT) aliibuka mshindi wa kuchora nembo hiyo ya Ukumbi wa Kimataifa wa
Mikutano wa Julius Nyerere (JNICC) kati ya washiriki 272.
“Ninaamini
kuwa katika shindano hili la kubuni nembo ya jengo hili la kimataifa
mimi nilikuwa wa mwisho kutuma kwani nilituma saa 1:45 usiku wa siku ya
deadline (siku ya mwisho),” anasema Abdallah.
Nikiwa mmoja wa waliohudhuria hafla ya uzinduzi wa nembo hiyo ya
jengo hilo la kimataifa wiki mbili zilizopita uliofanywa na Waziri wa
Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe, nilipata nafasi
ya kuzungumza na kijana huyo. Kijana huyo ambaye mara zote ni mcheshi
na akitaniana na ndugu pamoja na wanafunzi wenzake huku akionesha furaha
ya kuwa mshindi, anasema kuwa ushindi wake ni wa familia na kampuni
yake yenye wenzake watatu.
Abdallah ni kitinda mimba akiwa na pacha wake, Hannat, katika familia
ya mama Lulua Chandoma na baba Said Chandoma wenyeji wa Pemba katika
mji wa Zanzibar. Abdallah anasema alipata ushindani mkubwa katika
uchoraji wa nembo hiyo kutoka kwa marafiki zake huku akiungwa mkono na
wazazi wake.
Anabainisha kuwa katika shindano hilo aliweza kujinyakulia Sh milioni
tano na cheti maalumu, zawadi ambazo alisema anazipeleka katika kampuni
ikiwa ni moja ya hamasa kuongeza juhudi katika shughuli zake. Abdallah
anasema akiwa mdogo alipenda kuchora michoro mbalimbali lakini alipofika
kidato cha sita alianza kuchora picha kwa kutumia utaalamu wa kompyuta
ujulikanao kama Photoshop.
Anasema lakini alipofika chuo kikuu akiungana na wenzake wawili ambao
alisoma nao awali, waliamua kuanzisha kampuni na kutengeneza nembo,
‘banners’, mabango na stika mbalimbali huku wakiendelea na masomo.
Anasema mwaka huu walianza kutengeneza kwa kutumia utaalamu wa kwenye
kompyuta wa Illustrator ambao anakiri kuwa yote wanafanya kwa kipaji na
utundu kwani hawafundishwi popote shuleni.
“Uchoraji huu nimeufanya tangu mtoto na nimekuwa kila mara
nikijifunza mwenyewe, hivyo kwa kushirikiana na wenzangu mwaka jana
tuliamua kuanzisha kampuni yetu wenyewe,”anasema. Anawataja wenzake
katika kampuni yao iitwayo Alpha Arts akimaanisha kuwa sanaa wanayofanya
kwanza, ni Owen Patrik (23) wanayesoma naye IFM na Edwin Mmuni (23)
anayesoma chuo cha Arusha.
Akizungumzia jinsi wanavyofanya kazi huku mmoja akiwa Arusha anasema
mara nyingi hutumia simu kwa kupiga na wakati mwingine hutumia utaalamu
wa kujadili pamoja kwa simu kwa wakati mmoja (Conference Call). Anasema
kwa sasa wanamalizia usajili wa kampuni hiyo ambayo wamempa kazi
Mwanasheria kusimamia usajili kutokana na kuwa wao wako vyuoni huku
wakiendelea na kazi wanazopata kwenye kampuni yao.
Abdallah anasema wanatarajia ifikapo Aprili mwaka huu watazindua
rasmi kampuni yao pamoja na tovuti itakayoonesha kazi zao zote
walizowahi kufanya. Kushiriki Shindano la Nembo Abdallah anasema siku
tatu kabla ya kufikia tarehe ya mwisho ya shindano ndipo mmoja wa
marafiki zao aliwataarifu kuwepo wa shindano hilo na kuwataka kujaribu.
Anasema wote walipatwa na shauku ya kufanya hivyo lakini kutokana na
siku hiyo kuwa na kazi nyingine katika kampuni yao ambazo zilishalipiwa
na wateja zilitakiwa kuchukuliwa siku hiyo. Kutokana na hali hiyo,
kulitokea ubishani mkubwa baina yao ambapo wapo waliotaka kumalizia kazi
waliolipwa kwani ubunifu wa nembo ni kubahatisha tu huku yeye akiwataka
kufanya zote.
Mwisho yeye akikazania jambo lililowafanya wenzake kujitoa wakati
wameshaanza ubunifu wa awali kwa pamoja hivyo yeye akaamua kuendelea na
ubunifu wa nembo hiyo. Anasema wakati mwisho wa kupeleka nembo hizo za
ushindani ikiwa Desemba 31 mwaka jana, yeye siku ya Desemba 30 ndipo
alipofika na kuliona jengo lenyewe ambalo awali alikuwa halifahamu.
“Baada ya kuliona kwani awali nilitengeneza nembo yenye sura ya Baba
wa Taifa nikaamua kulibadilisha na kuweka picha ya jengo kama unavyoona
na kutengeneza mandhari ya Jiji la Dar es Salaam kwa kuweka mnazi na
alama ya bahari,” anasema. Alisisitiza kuwa alitengeneza akiwa na
madhumuni ya kujaribu tu kwani aliamini zipo kampuni kubwa
zitakazoshiriki hivyo yeye kuwa vigumu kushinda ikiwa ni mara yake ya
kwanza kushiriki katika shindano kama hilo.
Abdallah anasema akiwa na wenzake walituma mara 10 nembo hiyo baada
ya kukamilika siku hiyohiyo ya mwisho kuanzia saa 10 jioni hadi saa 1:45
usiku ilipokubali kwenda. “Siku hiyo, mtandao ulikuwa ukisumbua sana
kutokana na kuwa ni mwisho wa mwaka hivyo tulijaribu kutuma lakini
ilikuwa imekataa na mara nyingine nilikuwa nakata tamaa kabisa lakini
ilipofika muda huo ikakubali,”anasema.
Abdallah anasema kuwa baada ya kushinda shindano hilo amepata mwamko
na yuko tayari kushiriki mashindano yoyote yanayokuja mbele yake. Huku
akiwataka vijana wenzake kuwa tayari kujaribu na siyo kuogopa na kudhani
kuna watu maalum watashiriki masuala mbalimbali.
Anasema hata siku moja hakuwahi kutegemea kazi ya mikono yake
kutumika katika jengo kub- wa kama hilo ambalo linatambulika ndani na
nje ya nchi huku likibeba heshima ya jina la Baba wa Taifa. Anasema yeye
na pacha wake ni watoto wa mwisho kati ya saba wa baba na mama
Chandoma, wa kike wanne na wa kiume watatu.
Anasema familia hiyo inaishi Boko jijini Dar es Salaam huku pacha
wake akimaliza Diploma ya masuala ya Masoko na kufanya kazi katika
Kampuni ya Samsung. Anasema amesoma Shule ya Msingi Mwenge huku Kidato
cha kwanza hadi cha nne akisoma Shule ya Sekondari ya Dar es Salaam.
Anasema baadaye kidato cha tano na sita alisoma Sekondari ya Makongo
na kuchukua masomo ya HGE (Historia, Jiografia na Uchumi) kisha baadaye
kujiunga na IFM. Akimzungumzia Abdallah, mama yake mzazi Lulua Chandoma
anasema tangu akiwa mtoto mwanawe huyo alipenda kuchora mara kwa mara
kiasi ambacho kuta zote za nyumba na geti zilijaa michoro tofauti ya
ubunifu.
Anasema familia imepata furaha ya ajabu na kumtaka ajiendeleze zaidi
na wao kuendelea kumpa ushirikiano kwani katika shindano hilo alipeleka
nembo mbili na baba yake alimchagulia ile aliyoshinda. Naye Meneja wa
Ukumbi huo, Deus Kulwa anataja sifa za nembo iliyoshinda kuwa ni na
alama ya jengo lenyewe, rangi ya dhahabu inayoonesha hadhi ya jengo hilo
kuwa ni dhahabu.
Pili ni rangi ya bluu inayoonesha jengo lipo Pwani karibu na bahari,
anga ya dunia na mnazi ambao ni alama ya zao la Pwani. Akizungumza kwa
niaba ya Kampuni yao, Mmuni anasema suala hilo ni la kujivunia na
itatumika kutangaza kampuni hiyo ya vijana wadogo ambao wamethubutu kwa
nia ya kujiajiri.
Akizungumza wakati wa kuzindua nembo hiyo, Membe alisema kupitia
kituo hicho Serikali imejiandaa kuleta ulimwengu Tanzania na nembo hiyo
iwe chachu ya Watanzania wote kutumia kituo hicho kwa mikutano
mbalimbali, sherehe na hata zile za kijamii kama harusi.
“Ni vema Watanzania wote kuleta mikutano ya taasisi, kampuni za
kimataifa na hata sherehe mbalimbali ili kumuenzi Baba wa Taifa kwa
kutumia kituo hicho ambacho ni kitega uchumi cha Serikali,” anasema
Membe. Naye Mkurugenzi Mwendeshaji wa AICC, Elishilia Kaaya anasema
katika mchakato wa kupata nembo hiyo ilishirikisha Watanzania kwa
kutumia vyombo vya habari ambapo walishiriki Watanzania 272
waliowasilisha nembo za ubunifu 352.
Alisema nembo iliyoshinda ilionesha sura na mandhari ya kituo kilipo
huku wakiwa na mikakati ya kujenga vituo vingine kama hivyo Zanzibar na
Iringa ambacho kitawezesha ukanda wa Kusini kuwa na utalii wa mikutano.
Alisema kituo hicho kimekabidhiwa rasmi kwa uongozi wa Kituo cha
Mikutano cha Kimataifa cha Arusha (AICC) ili kukisimamia na uongozi huo
umedhamiria kituo hicho kutofunikwa na kivuli cha AICC kwa kukipatia
nembo yake stahili.
Kituo hicho kilizinduliwa Machi mwaka jana na Rais wa Jamhuri ya Watu
wa China, Xi Jinping, alipokuwa katika ziara yake ya kiserikali ya siku
mbili nchini. Jengo hilo limejengwa na Serikali China, ujenzi wake
umegharimu dola za Marekani milioni 29.7 (Sh bilioni 47.5) likiwa na
uwezo kuhodhi Mikutano minne kwa mara moja, yenye idadi ya watu 1,600.
Kituo hicho cha mikutano kipo kitalu namba 10 katika makutano ya
barabara za Garden na Shaaban Robert kikiwa kimejengwa na Serikali ya
Tanzania kwa kushirikiana na Serikali ya China. Kazi za kituo hicho ni
kuendesha mikutano, kutangaza vivutio vya utalii vinavyopatikana nchini
kupitia mikutano na kuangalia na kutunza majengo ya kituo hiki.
Katika kuendesha mikutano, kituo kina jumla ya kumbi 16 ambapo ukumbi
mkubwa kabisa una uwezo wa kuchukua hadi watu 1,003; kumbi za ukubwa wa
kati zenye uwezo kuchukua kati ya watu 150 mpaka watu 300, na kumbi
zingine ndogo 11 zenye uwezo wa kuchukua hadi watu 50 kila moja.
Pia Kituo kina kumbi kwa ajili ya sherehe mbalimbali kama harusi na
shughuli za burudani likiwepo eneo la juu la wazi na Lobby tatu ambazo
hutumika kwa ajili ya Mchapalo na wakati mwingine kwa ajili ya maonesho.
Kumbi zote za mikutano katika Kituo cha JNICC zimefungwa vifaa
mbalimbali vya kisasa vinavyosaidia kuwezesha mikutano kwenda vizuri.Chanzo Habari Leo
Subscribe to:
Posts (Atom)