Friday 7 March 2014

7 PICHAZ..MFAHAMU KIJANA ALIYEFANANA NA OBAMA KILA KITU...KAMA MAPACHA VILE...JIONEE MWENYEWE HAPA... 


 

Obama awasiliana na Putin kuhusu Ukraine

 

Mawasiliano kati ya Putin na Obama.
Rais Obama amefanya mazungumzo zaidi ya kina na rais wa Urusi Vladmir Putin akisistiza kuwa vitendo vya nchi yake katika jimbo la Crimea ni ukiukaji wa mipaka na uhuru wa taifa la Ukraine.
Wakati wa mazungumzo yao ya pili kupitia njia ya simu katika kipindi cha siku sita zilizopita, bwana Obama amependekeza njia ya kusuluhisha mzozo huo kidiplomasia inayojumuisha Urusi kuwaondoa wanajeshi wake katika jimbo la Crimea. Bwana Putin amesema uhusiano kati ya Moscow na Washington haufai kutatizika kutokana na mzozo wa Ukraine.
Awali bwana alisema kuwa kura ya maoni iliyopendekezwa kuhusu jimbo la Crimea kujiunga na Moscow inakiuka sheria ya kimataifa na sharti ijumuishe serikali ya Kiev iwapo itaandaliwa.
Akizungumza baada ya mkutano mwingine wa Baraza la Usalama uliofanyika faraghani, balozi wa Uingireza katika umoja wa mataifa , Mark Lyall Grant, amesema haiwezekani muafaka kupatikana katika baraza hilo kuhusu mzozo huo.
Bunge la Crimea limepiga kura kujitenga na Urusi.
"Nadhani hakuna dalili kwamba kutakuwa na mwafaka katika baraza la usalama katika kipindi cha siku chache zijazo. Kama ulivyosikia kutoka kwa wengine, kuna mashauri yanayoendelea kati ya wanadiplomasia kwenye mikutano mbali mbali Ulaya. Mashauri hayo yataendelea,'' amesema bwana Grant.
''Pengine kiwango fulani cha makubaliano kitaafikiwa ili kutuliza mgogoro huu na kisha baraza la usalama pengine litapata suluhu. Lakini hatujafutilia mbali mpango wa kuwasilisha azimio mbele ya Baraza la Usalama wakati wowote na tunafuatilia hali ya mambo kwa karibu tukitarajia baraza la Usalama likutane tena katika siku chache zijazo ikitegemea kitakachotokea mashinani."
Mzozo huo wa Ukraine umechochea wanasiasa pamoja na wageni wengine mashuhuri kususia mashindano ya Olimpiki ya wanariadha walemavu nchini Urusi. Marekani imeondoa ujumbe wake katika michezo hiyo na mawaziri wa Uingereza hawatakuwepo sawia na wenzao kutoka mataifa mengine ya Ulaya.

Wanadiplomasia watimuliwa Venezuela

Serikali ya Venezuela imemtimua Balozi wa Panama na wanadiplomasia wengine wakati huu kukiwa na maandamano ya upinzani nchini humo.

 

 Rais wa Venezuela,Nicolas Maduro

Maafisa hao walipewa saa 48 kuondoka nchini Venezuela.
Hatua hii imekuja siku moja baada ya Rais wa Venezuela, Nicolas Maduro kuvunja mahusiano ya kidiplomasia na kiuchumi na Panama.
Takriban watu 20 wameuawa wakati wa maandamano ya kuipinga serikali ya Venezuela mwezi uliopita.
Maduro ameishutumu Panama kupanga njama za kuiangusha serikali yake.
Raia wa Venezuela kwa muda mrefu wamekua wakilalamikia ongezeko la vitendo vya uhalifu, kupanda kwa gharama za maisha na ukosefu wa bidhaa muhimu.

 

Sasa malaria yakwea milima.

Kimelea kinachosababisha Malaria. Mbu hawapendi mazingira ya baridi.
Watafiti kutoka Uingereza na Marekani wanasema kuwa mabadiliko ya hali ya hewa huenda yakazua ongezeko kubwa la maambukizi ya ugonjwa wa Malaria kote duniani huku ugonjwa huo ukienea katika maeneo ya milimani barani Afrika na Amerika ya Kusini.
Katika matokeo ya utafiti yaliyochapishwa kwenye jarida la Science, wanasayansi hao wanasema hata ongezeko dogo katika viwango vya joto siku za usoni huenda likaongeza kwa mamilioni maambukizi ya malaria.
Mbu anayesababisha malaria.
Watafiti wamepata ushahidi kwamba mbu anayebeba kimelea kinachosababisha malaria wanaelekea katika nyanda za juu wakati viwango vya joto vikipanda.
Watu wanaoishi katika maeneo ya nyanda za juu wanakosa kinga na hivyo kurahisisha maradhi ya malaria kuenea.
Takriban watu milioni mia mbili ishirini kote duniani huambukizwa ukonjwa wa malaria.

Mnyika atishia kuwataja vigogo

Wakati huohuo, Waziri Kivuli wa Nishati na Madini, John Mnyika ametishia kuwataja kwa majina vigogo wa Serikali na CCM aliosema wako nyuma ya ‘kashfa’ kuhusu mgogoro huo ili waweze kuhojiwa kwa umma iwapo Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo hatajitokeza kufafanua kauli alizozitoa bungeni kutuhumu IPTL.
Mnyika ambaye pia ni Mbunge wa Ubungo (Chadema), alisema hayo katika taarifa yake kwa vyombo vya habari, akimtuhumu Waziri Muhongo kwa kudai bungeni Mei 25, 2013 kuwa yeye hakutumwa wizarani kupekua mafaili ili kufuatilia mlolongo wa kesi za IPTL.
Alisema anachukua hatua hiyo kwa kuzingatia kwamba madaraka na mamlaka ni ya wananchi... “Serikali inafanya kazi kwa niaba ya wananchi; hivyo pale Serikali inapochelewa kuchukua hatua kutokana na udhaifu, uzembe, ufisadi au uongo, ni muhimu wananchi wakashiriki kutaka uwajibikaji.”


Wavuvi: Mradi wa gesi unatupunguzia samaki baharini

  

Katika kipindi cha zaidi ya miaka miwili sasa upatikanaji wa samaki wa kitoweo katika pwani ya Bahari ya Hindi, eneo la Mkoa wa Mtwara, umekuwa mgumu.
Uchunguzi uliofanywa na mwandishi wa makala haya hivi karibuni, umebaini kuwa mabadiliko ya hali ya hewa na zana duni za uvuvi zinachangia hali hiyo.
Lakini wakazi wa Mtwara ambao baadhi yao wanategemea uvuvi, wanaamini kuwa upungufu wa samaki, umechangiwa na ongezeko kubwa la mahitaji ya samaki tofauti na uwezo wa wavuvi kulilisha soko la walaji.
Pamoja na wavuvi kukiri kuongezeka kwa soko la samaki, wanasema upatikanaji wake umekuwa mgumu hata kwa wale  wanaotumia zana nzuri katika uvuvi.
Wavuvi wanaamini kuwa uchimbaji wa nishati ya gesi asilia imesababisha mabadiliko ya hali ya hewa baharini kutokana na matumizi ya kemikali za kulipua ndani ya bahari wakati wa utafiti na uchimbaji.
“Hapo awali kabla ya kuanza uchimbaji wa gesi asilia baharini, tulikuwa na upepo wa matalai, upepo wa mlaji na upepo wa umande. Pepo hizo zilikuwa mwongozo kwetu kwenye  shughuli zetu za uvuvi,” anasema Ali Hamis Kimbaumbau,  mvuvi na mkazi wa mjini Mtwara.
Anafafanua kuwa pepo za matalai na umande ambazo ni upepo wa kusini huwa ni shwari na zikiambatana na upepo ambao ulikuwa unatoa fursa kwa wavuvi wanaotumia mitumbwi kwenda baharini. Kipindi hicho wavuvi walikuwa wanapata samaki ingawa si kwa kiwango kikubwa.
Anabainisha kuwa kwa sasa pepo wanazopata ni za kaskazi ambazo huambatana na upepo mkali, hali inayozuia wavuvi wenye mitumbwi isiyotumia mashine kushindwa kwenda baharini. Wavuvi wanaofanikiwa kwenda baharini hurudi na mapato duni.
Mvuvi mwingine, Salumu Liwanje (36) anasema wamefikia hatua ya kuamini utafiti na uchimbaji wa gesi asilia baharini ndiyo chanzo.
Anaeleza kuwa siku moja wakiwa baharini, eneo la Luvula walibaini nyaya zenye umeme baharini na walirushwa wakati walipojaribu kugusa maji hayo. Alisema baadaye walisikia sauti ya milipuko mara kadhaa hali waliyodai inaharibu mazingira ya asili ya bahari.
“Joto limeongezeka sana baharini. Hiyo  hali si ya kawaida, ukiingia bahari kuu utakutana na joto ambalo si la kawaida kabisa. Sisi tulizoea nyakati za usiku baharini kunakuwa na baridi kali, lakini hali ni kinyume kwa sasa,” anabainisha Liwanje.
“Unajua wengine tukisema mabadiliko tunayoyaona wapo, watakaosema ni walewale wasiopenda mradi wa gesi. Sasa sisi kama wavuvi tukigusa yale maji yaliyotandazwa nyaya tunarushwa na umeme, je samaki wataishi eneo hilo? ” anahoji mvuvi huyo.

Wafanyakazi Muhimbili walilia Sh800 mil zao

  

Dar es Salaam. Wafanyakazi wa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH) wameulalamikia uongozi wa hospitali hiyo kwa kushindwa kuwalipa fedha zao na kuzitumia kinyume na utaratibu uliopangwa.
Fedha zinazotajwa kutolipwa ni pamoja na Sh800 milioni za posho ya awamu ya tatu zinazotokana na mapato ya wateja wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya ambazo imedaiwa zilitumika kununulia vifaa tiba vya hospitali hiyo na fedha za likizo za tangu mwaka jana.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti wafanyakazi hao walisema hawajalipwa posho hizo tangu Januari, 2013 baada ya kuelezwa na mkurugenzi wa hospitali hiyo kuwa fedha hizo zitaelekezwa kununulia vifaa vya hospitali.
“Tunashindwa kuelewa hawa viongozi wetu! wanatumia fedha kwa maelekezo tofauti, hii inasababisha kuwapo na migogoro ndani ya kazi,” alisema mmoja wa wafanyakazi hao.
Mtoa habari huyo alisema wafanyakazi wameshangazwa na kauli ya Mkurugenzi Mkuu wa hospitali hiyo, Dk. Marina Njelekela kudai hawatalipwa posho na kwamba fedha hizo zitanunulia vifaa.
“Tunatakiwa kulipwa fedha hizo kama tahadhari. Mfano unaweza ukamuhudumia mgonjwa wa Ukimwi na ikatokea katika kumtibia akakuambukiza hela hii unayolipwa ndiyo kazi yake,” alisema.
Ofisa Uhusiano Mwandamizi wa hospitali hiyo, Aminiel Aligaesha alikiri uongozi wa MNH kutumia fedha hizo kwa matumizi mengine.
Waziri wa Afya na Ustawi wa jamii, Dk. Seif Rashid alisema alipata taarifa hizo na walikaa kikao na Bodi, mkurugenzi na chama cha Tughe kujadiliana suala hilo kwa kuwa ni la kisheria zaidi.
“Hili suala lipo kisheria zaidi. Niliwaagiza waende wakakae pamoja wajadiliane waweze kupata mwafaka ili wawalipe wafanyakazi hao,” Dk. Seif.

Ngumi mkononi bungeni

Mjumbe wa Bunge Maalumu la Katiba, Magdalena Sakaya (kushoto), akizozana na Magdalena Likwina baada ya Semina ya Kupitia Vifungu vya Rasimu ya Kanuni kuahirishwa kutokana na vurugu zilizotokea bungeni jana. Picha na Silvan Kiwale  

Dodoma. Ngumi mkononi ndilo neno jepesi ambalo linafaa kutumika baada ya vurugu kubwa kutokea jana ndani ya Ukumbi wa Bunge Maalumu la Katiba kiasi cha kumlazimisha Mwenyekiti wa Muda, Pandu Ameir Kificho kuahirisha semina kabla ya wakati wake.
Semina ya wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba, imekuwa ikianza saa 4:00 asubuhi hadi saa 7:00 mchana kabla ya kuendelea tena kuanzia saa 11:00 jioni hadi saa 3:00 usiku. Jana, katika kipindi cha asubuhi, semina hiyo iliahirishwa saa 6:17 licha ya kuanza saa tano asubuhi kabla ya kurejea tena saa 10 jioni.
Ngumi zilitaka kupigwa baada ya Waziri wa Katiba na Sheria wa Zanzibar, Abubakari Hamis Bakari kuhoji uhalali wa Christopher Ole Sendeka na Ummy Mwalimu kuchangia wakati hawakuwamo katika orodha ya wachangiaji jambo ambalo liliibua mjadala mkali na kurushiana maneno kabla ya Mwenyekiti Pandu Ameir Kificho kuahirisha semina hiyo.
Chanzo cha vurugu
Kificho alimpa Ole Sendeka nafasi ya kuchangia Kifungu namba 58 cha rasimu ya kanuni na baada ya kutoa mchango wake, Hamisi ambaye pia ni Mjumbe wa Kamati ya Kanuni, alisimama na kumtaka Mwenyekiti Kificho kuacha kuwateua watu ambao hawamo katika orodha ya wachangiaji.
Kificho hakumsikiliza na badala yake, alimpa nafasi mjumbe mwingine wa Bunge hilo Ummy Mwalimu ambaye pia ni Naibu Waziri, Ofisi ya Makamu wa Rais, kuchangia. Hata hivyo kabla hajafanya hivyo, Bakari alisimama tena na kumzuia kuchangia kwa madai kuwa hakuwamo kwenye orodha ya wachangiaji.
“Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tutaendelea na utaratibu huu suala la kuchangia kanuni linaweza kutupeleka hadi miezi sita bila ya kumaliza. Haya majina hayakuwemo kwenye orodha ya wachangiaji na huyo aliyemaliza sasa Ole Sendeka, naye hakuwamo, naomba tuache mchezo huu,” alisema Bakari.
Aliendelea: “Sekretarieti inakuchomekea majina mwenyekiti na kama hivyo ndivyo, basi tunatakiwa kuwachukulia hatua kali hawa kwani tunataka kujadili hoja ambazo hazimo.”
Bakari alisema wajumbe waliotakiwa kuchangia ni wale ambao walipeleka majina kwa makatibu wa Bunge hilo pamoja na michango yao kwa maandishi ili wapewe nafasi ya kuzungumza, lakini Kificho alikuwa akiwateua wajumbe ambao hawamo katika orodha hiyo.
Kificho ajibu
“Mimi sina tatizo na jambo hilo, mkisema tuendelee basi sawa, lakini mkitaka tufanye mambo kwa uzuri inawezekana pia, jambo la muhimu ni kuwa tupo hapa kutengeneza Katiba ya wananchi siyo ya vyama.”
Kelele zilianza kusikika huku wajumbe wakiimba kuwa mwenyekiti anayumba… na kumtaka mwenyekiti atoke nje na kukiacha kiti, kwani anafanya upendeleo.

 

Suleiman Abdallah: Mwanafunzi wa IFM aliyechora nembo ya ukumbi wa Julius Nyerere

SULEIMAN Abdallah (24) ni mwanafunzi wa Chuo cha Usimamizi wa Fedha (IFM) jijini Dar es Salaam ambaye hivi karibuni aliweka historia kwa kushinda kuchora nembo ya ukumbi maarufu jijini Dar es Salaam.
Abdallah anayechukua shahada ya Mawasiliano ya Habari na Teknolojia (ICT) aliibuka mshindi wa kuchora nembo hiyo ya Ukumbi wa Kimataifa wa Mikutano wa Julius Nyerere (JNICC) kati ya washiriki 272.

 “Ninaamini kuwa katika shindano hili la kubuni nembo ya jengo hili la kimataifa mimi nilikuwa wa mwisho kutuma kwani nilituma saa 1:45 usiku wa siku ya deadline (siku ya mwisho),” anasema Abdallah.
Nikiwa mmoja wa waliohudhuria hafla ya uzinduzi wa nembo hiyo ya jengo hilo la kimataifa wiki mbili zilizopita uliofanywa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe, nilipata nafasi ya kuzungumza na kijana huyo. Kijana huyo ambaye mara zote ni mcheshi na akitaniana na ndugu pamoja na wanafunzi wenzake huku akionesha furaha ya kuwa mshindi, anasema kuwa ushindi wake ni wa familia na kampuni yake yenye wenzake watatu.

Abdallah ni kitinda mimba akiwa na pacha wake, Hannat, katika familia ya mama Lulua Chandoma na baba Said Chandoma wenyeji wa Pemba katika mji wa Zanzibar. Abdallah anasema alipata ushindani mkubwa katika uchoraji wa nembo hiyo kutoka kwa marafiki zake huku akiungwa mkono na wazazi wake.

Anabainisha kuwa katika shindano hilo aliweza kujinyakulia Sh milioni tano na cheti maalumu, zawadi ambazo alisema anazipeleka katika kampuni ikiwa ni moja ya hamasa kuongeza juhudi katika shughuli zake. Abdallah anasema akiwa mdogo alipenda kuchora michoro mbalimbali lakini alipofika kidato cha sita alianza kuchora picha kwa kutumia utaalamu wa kompyuta ujulikanao kama Photoshop.

Anasema lakini alipofika chuo kikuu akiungana na wenzake wawili ambao alisoma nao awali, waliamua kuanzisha kampuni na kutengeneza nembo, ‘banners’, mabango na stika mbalimbali huku wakiendelea na masomo. Anasema mwaka huu walianza kutengeneza kwa kutumia utaalamu wa kwenye kompyuta wa Illustrator ambao anakiri kuwa yote wanafanya kwa kipaji na utundu kwani hawafundishwi popote shuleni.
“Uchoraji huu nimeufanya tangu mtoto na nimekuwa kila mara nikijifunza mwenyewe, hivyo kwa kushirikiana na wenzangu mwaka jana tuliamua kuanzisha kampuni yetu wenyewe,”anasema. Anawataja wenzake katika kampuni yao iitwayo Alpha Arts akimaanisha kuwa sanaa wanayofanya kwanza, ni Owen Patrik (23) wanayesoma naye IFM na Edwin Mmuni (23) anayesoma chuo cha Arusha.

Akizungumzia jinsi wanavyofanya kazi huku mmoja akiwa Arusha anasema mara nyingi hutumia simu kwa kupiga na wakati mwingine hutumia utaalamu wa kujadili pamoja kwa simu kwa wakati mmoja (Conference Call). Anasema kwa sasa wanamalizia usajili wa kampuni hiyo ambayo wamempa kazi Mwanasheria kusimamia usajili kutokana na kuwa wao wako vyuoni huku wakiendelea na kazi wanazopata kwenye kampuni yao.
Abdallah anasema wanatarajia ifikapo Aprili mwaka huu watazindua rasmi kampuni yao pamoja na tovuti itakayoonesha kazi zao zote walizowahi kufanya. Kushiriki Shindano la Nembo Abdallah anasema siku tatu kabla ya kufikia tarehe ya mwisho ya shindano ndipo mmoja wa marafiki zao aliwataarifu kuwepo wa shindano hilo na kuwataka kujaribu.

Anasema wote walipatwa na shauku ya kufanya hivyo lakini kutokana na siku hiyo kuwa na kazi nyingine katika kampuni yao ambazo zilishalipiwa na wateja zilitakiwa kuchukuliwa siku hiyo. Kutokana na hali hiyo, kulitokea ubishani mkubwa baina yao ambapo wapo waliotaka kumalizia kazi waliolipwa kwani ubunifu wa nembo ni kubahatisha tu huku yeye akiwataka kufanya zote.

Mwisho yeye akikazania jambo lililowafanya wenzake kujitoa wakati wameshaanza ubunifu wa awali kwa pamoja hivyo yeye akaamua kuendelea na ubunifu wa nembo hiyo. Anasema wakati mwisho wa kupeleka nembo hizo za ushindani ikiwa Desemba 31 mwaka jana, yeye siku ya Desemba 30 ndipo alipofika na kuliona jengo lenyewe ambalo awali alikuwa halifahamu.

“Baada ya kuliona kwani awali nilitengeneza nembo yenye sura ya Baba wa Taifa nikaamua kulibadilisha na kuweka picha ya jengo kama unavyoona na kutengeneza mandhari ya Jiji la Dar es Salaam kwa kuweka mnazi na alama ya bahari,” anasema. Alisisitiza kuwa alitengeneza akiwa na madhumuni ya kujaribu tu kwani aliamini zipo kampuni kubwa zitakazoshiriki hivyo yeye kuwa vigumu kushinda ikiwa ni mara yake ya kwanza kushiriki katika shindano kama hilo.

Abdallah anasema akiwa na wenzake walituma mara 10 nembo hiyo baada ya kukamilika siku hiyohiyo ya mwisho kuanzia saa 10 jioni hadi saa 1:45 usiku ilipokubali kwenda. “Siku hiyo, mtandao ulikuwa ukisumbua sana kutokana na kuwa ni mwisho wa mwaka hivyo tulijaribu kutuma lakini ilikuwa imekataa na mara nyingine nilikuwa nakata tamaa kabisa lakini ilipofika muda huo ikakubali,”anasema.

Abdallah anasema kuwa baada ya kushinda shindano hilo amepata mwamko na yuko tayari kushiriki mashindano yoyote yanayokuja mbele yake. Huku akiwataka vijana wenzake kuwa tayari kujaribu na siyo kuogopa na kudhani kuna watu maalum watashiriki masuala mbalimbali.

Anasema hata siku moja hakuwahi kutegemea kazi ya mikono yake kutumika katika jengo kub- wa kama hilo ambalo linatambulika ndani na nje ya nchi huku likibeba heshima ya jina la Baba wa Taifa. Anasema yeye na pacha wake ni watoto wa mwisho kati ya saba wa baba na mama Chandoma, wa kike wanne na wa kiume watatu.

Anasema familia hiyo inaishi Boko jijini Dar es Salaam huku pacha wake akimaliza Diploma ya masuala ya Masoko na kufanya kazi katika Kampuni ya Samsung. Anasema amesoma Shule ya Msingi Mwenge huku Kidato cha kwanza hadi cha nne akisoma Shule ya Sekondari ya Dar es Salaam.

Anasema baadaye kidato cha tano na sita alisoma Sekondari ya Makongo na kuchukua masomo ya HGE (Historia, Jiografia na Uchumi) kisha baadaye kujiunga na IFM. Akimzungumzia Abdallah, mama yake mzazi Lulua Chandoma anasema tangu akiwa mtoto mwanawe huyo alipenda kuchora mara kwa mara kiasi ambacho kuta zote za nyumba na geti zilijaa michoro tofauti ya ubunifu.

Anasema familia imepata furaha ya ajabu na kumtaka ajiendeleze zaidi na wao kuendelea kumpa ushirikiano kwani katika shindano hilo alipeleka nembo mbili na baba yake alimchagulia ile aliyoshinda. Naye Meneja wa Ukumbi huo, Deus Kulwa anataja sifa za nembo iliyoshinda kuwa ni na alama ya jengo lenyewe, rangi ya dhahabu inayoonesha hadhi ya jengo hilo kuwa ni dhahabu.

Pili ni rangi ya bluu inayoonesha jengo lipo Pwani karibu na bahari, anga ya dunia na mnazi ambao ni alama ya zao la Pwani. Akizungumza kwa niaba ya Kampuni yao, Mmuni anasema suala hilo ni la kujivunia na itatumika kutangaza kampuni hiyo ya vijana wadogo ambao wamethubutu kwa nia ya kujiajiri.

Akizungumza wakati wa kuzindua nembo hiyo, Membe alisema kupitia kituo hicho Serikali imejiandaa kuleta ulimwengu Tanzania na nembo hiyo iwe chachu ya Watanzania wote kutumia kituo hicho kwa mikutano mbalimbali, sherehe na hata zile za kijamii kama harusi.
“Ni vema Watanzania wote kuleta mikutano ya taasisi, kampuni za kimataifa na hata sherehe mbalimbali ili kumuenzi Baba wa Taifa kwa kutumia kituo hicho ambacho ni kitega uchumi cha Serikali,” anasema Membe. Naye Mkurugenzi Mwendeshaji wa AICC, Elishilia Kaaya anasema katika mchakato wa kupata nembo hiyo ilishirikisha Watanzania kwa kutumia vyombo vya habari ambapo walishiriki Watanzania 272 waliowasilisha nembo za ubunifu 352.

Alisema nembo iliyoshinda ilionesha sura na mandhari ya kituo kilipo huku wakiwa na mikakati ya kujenga vituo vingine kama hivyo Zanzibar na Iringa ambacho kitawezesha ukanda wa Kusini kuwa na utalii wa mikutano. Alisema kituo hicho kimekabidhiwa rasmi kwa uongozi wa Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Arusha (AICC) ili kukisimamia na uongozi huo umedhamiria kituo hicho kutofunikwa na kivuli cha AICC kwa kukipatia nembo yake stahili.

Kituo hicho kilizinduliwa Machi mwaka jana na Rais wa Jamhuri ya Watu wa China, Xi Jinping, alipokuwa katika ziara yake ya kiserikali ya siku mbili nchini. Jengo hilo limejengwa na Serikali China, ujenzi wake umegharimu dola za Marekani milioni 29.7 (Sh bilioni 47.5) likiwa na uwezo kuhodhi Mikutano minne kwa mara moja, yenye idadi ya watu 1,600.

Kituo hicho cha mikutano kipo kitalu namba 10 katika makutano ya barabara za Garden na Shaaban Robert kikiwa kimejengwa na Serikali ya Tanzania kwa kushirikiana na Serikali ya China. Kazi za kituo hicho ni kuendesha mikutano, kutangaza vivutio vya utalii vinavyopatikana nchini kupitia mikutano na kuangalia na kutunza majengo ya kituo hiki.

Katika kuendesha mikutano, kituo kina jumla ya kumbi 16 ambapo ukumbi mkubwa kabisa una uwezo wa kuchukua hadi watu 1,003; kumbi za ukubwa wa kati zenye uwezo kuchukua kati ya watu 150 mpaka watu 300, na kumbi zingine ndogo 11 zenye uwezo wa kuchukua hadi watu 50 kila moja.
Pia Kituo kina kumbi kwa ajili ya sherehe mbalimbali kama harusi na shughuli za burudani likiwepo eneo la juu la wazi na Lobby tatu ambazo hutumika kwa ajili ya Mchapalo na wakati mwingine kwa ajili ya maonesho. Kumbi zote za mikutano katika Kituo cha JNICC zimefungwa vifaa mbalimbali vya kisasa vinavyosaidia kuwezesha mikutano kwenda vizuri.Chanzo Habari Leo