Friday 7 March 2014

Wafanyakazi Muhimbili walilia Sh800 mil zao

  

Dar es Salaam. Wafanyakazi wa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH) wameulalamikia uongozi wa hospitali hiyo kwa kushindwa kuwalipa fedha zao na kuzitumia kinyume na utaratibu uliopangwa.
Fedha zinazotajwa kutolipwa ni pamoja na Sh800 milioni za posho ya awamu ya tatu zinazotokana na mapato ya wateja wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya ambazo imedaiwa zilitumika kununulia vifaa tiba vya hospitali hiyo na fedha za likizo za tangu mwaka jana.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti wafanyakazi hao walisema hawajalipwa posho hizo tangu Januari, 2013 baada ya kuelezwa na mkurugenzi wa hospitali hiyo kuwa fedha hizo zitaelekezwa kununulia vifaa vya hospitali.
“Tunashindwa kuelewa hawa viongozi wetu! wanatumia fedha kwa maelekezo tofauti, hii inasababisha kuwapo na migogoro ndani ya kazi,” alisema mmoja wa wafanyakazi hao.
Mtoa habari huyo alisema wafanyakazi wameshangazwa na kauli ya Mkurugenzi Mkuu wa hospitali hiyo, Dk. Marina Njelekela kudai hawatalipwa posho na kwamba fedha hizo zitanunulia vifaa.
“Tunatakiwa kulipwa fedha hizo kama tahadhari. Mfano unaweza ukamuhudumia mgonjwa wa Ukimwi na ikatokea katika kumtibia akakuambukiza hela hii unayolipwa ndiyo kazi yake,” alisema.
Ofisa Uhusiano Mwandamizi wa hospitali hiyo, Aminiel Aligaesha alikiri uongozi wa MNH kutumia fedha hizo kwa matumizi mengine.
Waziri wa Afya na Ustawi wa jamii, Dk. Seif Rashid alisema alipata taarifa hizo na walikaa kikao na Bodi, mkurugenzi na chama cha Tughe kujadiliana suala hilo kwa kuwa ni la kisheria zaidi.
“Hili suala lipo kisheria zaidi. Niliwaagiza waende wakakae pamoja wajadiliane waweze kupata mwafaka ili wawalipe wafanyakazi hao,” Dk. Seif.

No comments:

Post a Comment