Friday 7 March 2014

Wavuvi: Mradi wa gesi unatupunguzia samaki baharini

  

Katika kipindi cha zaidi ya miaka miwili sasa upatikanaji wa samaki wa kitoweo katika pwani ya Bahari ya Hindi, eneo la Mkoa wa Mtwara, umekuwa mgumu.
Uchunguzi uliofanywa na mwandishi wa makala haya hivi karibuni, umebaini kuwa mabadiliko ya hali ya hewa na zana duni za uvuvi zinachangia hali hiyo.
Lakini wakazi wa Mtwara ambao baadhi yao wanategemea uvuvi, wanaamini kuwa upungufu wa samaki, umechangiwa na ongezeko kubwa la mahitaji ya samaki tofauti na uwezo wa wavuvi kulilisha soko la walaji.
Pamoja na wavuvi kukiri kuongezeka kwa soko la samaki, wanasema upatikanaji wake umekuwa mgumu hata kwa wale  wanaotumia zana nzuri katika uvuvi.
Wavuvi wanaamini kuwa uchimbaji wa nishati ya gesi asilia imesababisha mabadiliko ya hali ya hewa baharini kutokana na matumizi ya kemikali za kulipua ndani ya bahari wakati wa utafiti na uchimbaji.
“Hapo awali kabla ya kuanza uchimbaji wa gesi asilia baharini, tulikuwa na upepo wa matalai, upepo wa mlaji na upepo wa umande. Pepo hizo zilikuwa mwongozo kwetu kwenye  shughuli zetu za uvuvi,” anasema Ali Hamis Kimbaumbau,  mvuvi na mkazi wa mjini Mtwara.
Anafafanua kuwa pepo za matalai na umande ambazo ni upepo wa kusini huwa ni shwari na zikiambatana na upepo ambao ulikuwa unatoa fursa kwa wavuvi wanaotumia mitumbwi kwenda baharini. Kipindi hicho wavuvi walikuwa wanapata samaki ingawa si kwa kiwango kikubwa.
Anabainisha kuwa kwa sasa pepo wanazopata ni za kaskazi ambazo huambatana na upepo mkali, hali inayozuia wavuvi wenye mitumbwi isiyotumia mashine kushindwa kwenda baharini. Wavuvi wanaofanikiwa kwenda baharini hurudi na mapato duni.
Mvuvi mwingine, Salumu Liwanje (36) anasema wamefikia hatua ya kuamini utafiti na uchimbaji wa gesi asilia baharini ndiyo chanzo.
Anaeleza kuwa siku moja wakiwa baharini, eneo la Luvula walibaini nyaya zenye umeme baharini na walirushwa wakati walipojaribu kugusa maji hayo. Alisema baadaye walisikia sauti ya milipuko mara kadhaa hali waliyodai inaharibu mazingira ya asili ya bahari.
“Joto limeongezeka sana baharini. Hiyo  hali si ya kawaida, ukiingia bahari kuu utakutana na joto ambalo si la kawaida kabisa. Sisi tulizoea nyakati za usiku baharini kunakuwa na baridi kali, lakini hali ni kinyume kwa sasa,” anabainisha Liwanje.
“Unajua wengine tukisema mabadiliko tunayoyaona wapo, watakaosema ni walewale wasiopenda mradi wa gesi. Sasa sisi kama wavuvi tukigusa yale maji yaliyotandazwa nyaya tunarushwa na umeme, je samaki wataishi eneo hilo? ” anahoji mvuvi huyo.

No comments:

Post a Comment