Monday 24 March 2014

Ikulu: Kujadili hotuba ya JK kupoteza muda

Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais Ikulu, Salva Rweyemamu

Dar es Salaam. Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais Ikulu, Salva Rweyemamu amesema kuendelea kuijadili hotuba ya Rais Jakaya Kikwete aliyotoa kwenye Bunge la Katiba mwishoni mwa wiki ni kupoteza muda.
Akizungumza na gazeti hili jana, Rweyemamu aliushangaa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) kuendelea kutoa matamko yanayoipinga hotuba hiyo, akisema haumtendei haki mkuu huyo wa nchi na Watanzania wote kwa ujumla. Alisema kama Mtanzania, Rais alitoa maoni yake na amekuwa muungwana kwa kuwaambia kwamba bado wana fursa ya kujadili na kuleta mapendekezo yao, lakini wajali zaidi masilahi ya taifa.
“Hiyo ni propaganda isiyokuwa na maana kwa taifa na hata hatima ya Katiba yenyewe. Ningependa kuwakumbusha kwamba Watanzania wamewapeleka Dodoma wakajadili Katiba na siyo kufanya propaganda, tunawataka wafanye kazi,” alisema Rweyemamu.
Kwa mujibu wa Rweyemamu, umoja huo wenye viongozi kutoka vyama vya upinzani haumtendei haki Rais kwani kama Mtanzania, mkuu huyo wa nchi ana fursa ya kutoa maoni yake.
“Wasifikiri kwa kumjibu hivyo Rais wanajibizana na CCM. Rais ni mkuu wa nchi ana maoni yake, lakini zaidi ya yote, Bunge la Katiba siyo mahali pa kufanya siasa. Kama wanataka siasa tunawaomba warudi maofisini mwao wakafanye siasa, pale tumewatuma kazi,” alisisitiza.
Rweyemamu alibainisha kuwa mchakato wa kutunga Katiba unahitaji busara na busara hiyo haiwezi kupatikana kama watu waliotumwa kuwawakilisha wananchi wameamua kufanya siasa.
“Tunahitaji watu wote wawe CCM, CUF, Chadema na vyama vingine waache siasa,” alisema.
Wakati huohuo, bungeni Dodoma limeibuka kundi la wajumbe, wengi wao kutoka CCM wakiipongeza hotuba hiyo ya Rais Jakaya Kikwete na kuwakosoa watu wanaotishia kumpeleka Rais mahakamani kwa madai ya kuvunja kanuni na Sheria ya Mabadiliko ya Katiba kwa kuingilia mchakato wa maoni.
Mjumbe wa kundi hilo linalojiita Tanzania Kwanza, Evod Mmanda alisema siyo kweli kuwa Rais amevunja sheria kwani alihutubia Bunge baada ya kupitishwa kwenye kanuni za Bunge kifungu cha 75(1) ambacho kinaeleza mwenyekiti anaweza kumwalika mgeni rasmi kulihutubia Bunge.
Walioambatana na Mmanda ni Dk Emmanuel Nchimbi, Said Nkumba, Mohamed Thabit Kombo, Waride Jabu, Seleman Jafo na Charles Mwijage.

No comments:

Post a Comment