Monday 24 February 2014

TANZANIA KUPELEKA MAJESHI SUDAN KUSINI 

 Mzinga 3c649

Serikali inatarajia kupeleka kikosi kimoja cha Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) huko Sudan Kusini kwa ajili ya kulinda amani kutokana na vita ya wenyewe kwa wenyewe inayoendelea.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe anasema Dar es Salaam jana kwamba Serikali imekubali kupeleka batalioni moja baada ya kuombwa na Umoja wa Mataifa (UN).
Sudan ya Kusini imekuwa katika machafuko ambayo yamesababisha vifo vya mamia ya raia na wengine kujeruhiwa.
"Tumefanya uamuzi wa kupeleka majeshi yetu Sudan Kusini, tumefanya hivyo baada ya kuombwa na Umoja wa Mataifa kwa sababu ya ubora wa jeshi letu," Membe aliwaambia waandishi wa habari.
Anasema jukumu la kulinda amani katika Bara la Afrika ni la Waafrika wenyewe na kwamba Tanzania inajiona kwamba ina jukumu la kusaidia kupatikana kwa amani.
Anasema Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki-Moon alimwomba Rais Jakaya Kikwete kusaidia kupeleka majeshi yake Sudan Kusini kusaidia kulinda amani. "Rais alikubali, sasa tuko kwenye maandalizi, nadhani Aprili jeshi letu litaondoka kuelekea Sudan Kusini," alisema Membe.

Kwa sasa Tanzania ina vikosi vya wanajeshi wa kulinda amani katika nchi za DRC, Darfur (Sudan) na Lebanon. Chanzo: mwananchi


No comments:

Post a Comment