Tuesday 11 March 2014

Askofu Mtetemela awatuliza wananchi

Dodoma. Askofu Mkuu Mstaafu wa Kanisa la Anglikana Tanzania, Donald Mtetemela amewahakikishia Watanzania kuwa Katiba itapatikana kwa wakati.
Hata hivyo, amesema kuna haja kwa Watanzania wa dini zote kuliombea Bunge Maalumu la Katiba lifanye mambo kwa kumshirikisha Mwenyezi Mungu ili mchakato wa Katiba uende vizuri.
Askofu Mtetemela, ambaye ni mmoja wa mjumbe wa Bunge hilo, alitoa ushauri huo jana kwenye viwanja vya Bunge mjini Dodoma.
Alisema kuyumba kwa Bunge la Katiba kwa sasa kunatokana na misimamo ya vyama vya siasa na kwamba kitendo hicho kimesababisha kuchelewa kwa kazi ya msingi.
“Mambo ya misimamo hayawezi kuzuilika na wala si kosa kila kikundi kuwa na msimamo wake, lakini kinachotakiwa ni wajumbe kufuta mambo ya vyama vichwani mwao na hasa pale panapokuwa na hoja ya msingi,” alisema kiongozi huyo wa kiroho.
“Watanzania waendelee kutuombea kwa nguvu zote. Sina shaka tutatoka hapa tukiwa wamoja kwa sababu tunaimba wimbo mmoja wa kutaka kitu kizuri mbele yetu,” alisisitiza Askofu Mtetemela.
Askofu Mtetemela alisema kuwa katika hatua za awali kulikuwa na misukosuko mikubwa ndani ya Bunge, lakini sasa kuna mwelekeo wa kuridhisha kutokana na wajumbe kuelewa wajibu wao katika mchakato huu.

 

No comments:

Post a Comment