Tuesday 11 March 2014

Bunge Maalumu la Katiba sasa vululu vululu

 

Dodoma. Matarajio ya Bunge Maalumu la Katiba kukamilisha kanuni kwa maridhiano yaliyeyuka tena jana huku mambo ndani ya ukumbi yakionekana kuwa vululuvululu kwa baadhi ya wajumbe kuzungumza nje ya utaratibu na wengine kurushiana vijembe.
Baadhi ya wajumbe waliamua kutoleana lugha chafu na kuweka kando hoja za msingi zinazowafanya watofautiane na kuchelewesha kazi ya kuandika Katiba Mpya.
Hali ilichafuka mchana wakati wajumbe walipokutana kupitisha kanuni baada ya mmoja wao, Felix Mkosamali kuomba mwongozo kwa Mwenyekiti wa muda, Pandu Ameir Kificho. Hata hivyo, Kificho alimtaka kukaa chini kwa muda kwa maelezo kuwa wajumbe waliofika katika kikao hicho walikuwa wachache, hivyo mwongozo wake kama ulikuwa unahitaji majibu ingekuwa vigumu kutolewa.
Baada ya muda alisimama, James Mbatia na kuomba mwongozo, akihoji sababu za kutaka kuanza kikao cha kupitisha kanuni hizo wakati wajumbe hawajapewa vitabu vya rasimu ya kanuni zenyewe.
“Mwenyekiti ulitangaza asubuhi kuwa tutagawiwa kanuni kabla ya saa tisa lakini hadi sasa tunataka kusomewa kanuni wakati hatujagawiwa kanuni hizo,” alihoji Mbatia.
Kificho alitoa ufafanuzi kuwa kanuni hizo zilikuwa bado zinadurufiwa na kuwataka wajumbe wawe na nidhamu kwani anapotangaza wanapiga kelele.
Ghafla alisimama Mkosamali tena na kuwasha kipaza sauti na kuhoji kitendo cha mwenyekiti huyo kumpa Mbatia nafasi ya kutoa mwongozo wakati yeye amenyimwa... “Mwenyekiti hivi unaongozaje kikao, inakuwaje mimi nikuombe mwongozo uninyime na mwenzangu umpe? Mwenyekiti nakuheshimu sana, lakini sijui unatumia kanuni ipi kutoa nafasi kwa mjumbe wakati mimi ulinizuia nisiseme,” alihoji Mkosamali.
Baada ya kauli hiyo Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Hawa Ghasia aliwasha kipaza sauti na kwa sauti ya juu alisema “Mtoto mdogo hana adabu.” Kauli hiyo iliibua hasira za Mjumbe mwingine, Moses Machali ambaye naye aliwasha kipaza sauti na kumjibu: “Kubwa jinga halina adabu,” kauli iliyoibua miguno ndani ya Bunge.
Hata hivyo, licha ya Mwenyekiti kutoa onyo kwa kauli hizo kwamba hazifai, Mkosamali alisimama katika sehemu yake na kusema kuwa hakuna mtoto mdogo na kwamba tangu lini mtoto aliishinda CCM.
Chanzo cha tatizo
Chanzo cha mvurugano huo ambao wiki iliyopita kidogo usababishe ngumi kurushwa bungeni, ni mfumo wa upigaji kura katika kupitisha ibara za rasimu, ambao jana uliendelea kuwagawa wajumbe na kufanya ukumbi huo kuonekana kama eneo la mzaha.
Kauli za ‘ndiyoooo’, ‘hapanaaaa’ na vitendo vya kugonga meza viliongezeka katika kipindi cha asubuhi baada ya Mwenyekiti wa Kamati ya Kuandaa Kanuni, Profesa Costa Mahalu kuwaleza wajumbe kuwa kamati yake haijafikia mwafaka wa ama iwe kura za siri au wazi na kwamba suala hilo limerejeshwa kwa wajumbe wenyewe.

 

No comments:

Post a Comment