Kardinali Pengo aweka wazi msimamo wa Kanisa
Askofu Mkuu wa Kanisa Katoliki Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Muadhama Polycarp Kardinali Pengo akiwaonesha waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, nakala ya gazeti la Mwanachi lililoandika habari kuhusu msimamo wa Kanisa juu ya suala la serikali tatu. Picha na Venance Nestory
Dar es Salaam/Iringa. Siku mbili baada ya Tume
ya Haki na Amani ya Baraza la Maaskofu Tanzania (TEC) kutoa waraka wa
kulitaka Bunge Maalumu la Katiba kutopuuza mapendekezo ya muundo wa
serikali tatu, Askofu Mkuu wa Jimbo Mkuu la Dar es Salaam, Mwadhama
Polycarp Kardinali Pengo ameibuka na kusema msimamo huo siyo wa Kanisa
Katoliki nchini.
Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam
jana, Kardinali Pengo pamoja na kukiri kuwa tume ilitoa maoni hayo,
alikanusha kuwa taarifa zilizotolewa na moja ya magazeti kuwa msimamo wa
Kanisa Katoliki ni serikali tatu.
“Maoni ya Tume hayawezi kuwa ni msimamo wa kanisa.
Kanisa Katoliki lina utaratibu wa kutoa misimamo yake na huwa inatolewa
na Mwenyekiti wa TEC,” alisema.
Hata hivyo, Rais wa TEC, Askofu Tarcisius
Ngalalekumtwa kutoka Jimbo la Iringa, alisema jana kuwa alikuwa na
shughuli nyingi, hivyo asingeweza kuzungumzia suala hilo, labda wiki
ijayo.
Akizungumza katika makazi yake mjini Iringa,
Askofu Ngalalekumtwa alisema: “Mniache, nina shughuli nyingi…labda
mnitafute wiki ijayo,” alisema.
Vilevile, Pengo ambaye alirejea msimamo wake
binafsi wa kuunga mkono Muungano wa serikali mbili, alisema kwa namna
Rasimu ya Katiba ilivyo, hakuna kigezo cha kulazimisha Kanisa Katoliki
litoe msimamo.
Alisema Kanisa Katoliki lingeweza kutoa msimamo iwapo Rasimu ya Katiba ingekuwa na dosari zinazohusu imani au maadili.
“Kwa mfano, (Rasimu) ingekuwa inasema, hakuna
Mungu lazima tungekuja juu kwa sababu inaingilia imani yetu,” alisema
Kardinali Pengo na kufafanua:
“Vilevile tungeweza kusema inakwenda kinyume na maadili iwapo inaruhusu kuua wazee au inaunga mkono ndoa za jinsi moja.”
Tamko la Tume
Tamko la tume hiyo inayoongozwa na Askofu Mkuu wa
Tabora, Paulo Ruzoka liliweka bayana kuwa muundo wa serikali mbili
haukutatua matatizo ya msingi na badala yake ulilimbikiza kero
zilizosababisha Zanzibar kujiundia katiba yake mwaka 2010 bila
kushauriana na Tanzania Bara.
Tamko hilo la kurasa 15 lililosambazwa kwa baadhi
ya Wajumbe wa Bunge la Katiba, lilitolewa baada ya mkutano wa kitaifa wa
Wajumbe wa Kamati za Majimbo za Haki na Amani za Kanisa hilo na Chama
cha Wanataaluma Wakatoliki Tanzania (CPT), uliofanyika jijini Dar es
Salaam Februari 5 na 6 mwaka huu.
No comments:
Post a Comment