Tuesday 4 March 2014

Wamisri wainyima ulaji Yanga 

Mshambuliaji wa Yanga, Didier Kavumbagu (jezi ya kijani) akiwania mpira na mabeki wa Al Ahly wakati wa mchezo wa Ligi ya Mabingwa Afrika uliozikutanisha timu hizo kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, Jumamosi iliyopita. Yanga ilishinda 1-0. Picha na Michael Matemanga.  

Dar es Salaam. Klabu ya Yanga imepoteza dola 70,000 za Kimarekani (Sh 111.2 milioni) baada ya kampuni ya MGB ya Misri kushindwa kurusha moja kwa moja ‘Live’ mechi kati ya timu hiyo na Al Ahly iliyochezwa Uwanja wa Taifa mwishoni mwa wiki iliyopita.
Awali, Yanga iliingia mkataba wa Dola za Marekani 90,000 na kampuni hiyo kwa ajili ya kuonyesha mechi hiyo ya kwanza ya raundi ya kwanza ya Ligi ya Mabingwa Afrika kuwania kucheza raundi ya pili na ikapewa malipo ya awali dola 20,000.
Mwakilishi wa Kampuni ya MGB, Francis Gaitho aliuambia mtandao wa Al Ahly.com kuwa wanailaumu Yanga kwa kukwamisha zoezi la kurusha mechi hiyo, akidai waliwafukuza uwanjani wafanyakazi wa televisheni ya Star TV na kamera zao waliokwenda kurusha moja kwa moja pambano hilo.
Alisema baada ya kusaini mkataba na Yanga, waliwalipa fedha za awali kutoka kwenye akaunti yao nchini Misri kwenda kwenye akaunti ya klabu hiyo Tanzania.
Gaitho alisema timu ya watu wa utayarishaji waliotakiwa kuja Dar es Salaam kurekodi mchezo huo ilishindwa kufika kwa wakati kutoka Cairo, hivyo wakalazimika kutafuta kampuni ya Tanzania kufanya kazi hiyo na Star TV ya Tanzania ikabahatika kupata zabuni kutoka kwao.
Alisema kuwa licha wa ubalozi wa Misri nchini Tanzania kuiandikia barua klabu ya Yanga kwamba MGB italipa malipo yaliyobaki baada ya mechi na kudhaminiwa na Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Jamal Malinzi, uongozi wa Yanga iligoma kurekodiwa  kwa mechi hiyo.
“Wakati tulipofikia mwafaka na kukubaliana mechi irekodiwe, kwa bahati mbaya Star TV walikuwa tayari wamekwishaondoka uwanjani na muda ulikuwa umeenda,” alisema Gaitho.
Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Mashindano ya Yanga, Mussa Katabaro akizungumzia madai hayo katika mahojiano na mtandao wa Bin Zubery alikiri klabu hiyo kupokea malipo ya Dola 20,000 na kudai kuwa klabu yake ilipaswa kulipwa kiasi kingine cha Dola 35,000 kabla ya mechi na Dola 35,000 nyingine baada ya mechi, lakini MGB ilishindwa kutekeleza kipengele hicho cha mkataba. “Mbaya zaidi, katika mkataba wetu na wao tulikubaliana hakuna kupelekana mahakamani, sasa tulipoona wameshindwa kulipa zile fedha.
Katabaro alisema wateja wao hawakuwa wa kweli katika maelezo yao baada ya kudai kwamba kuna mtu alikuwa anakuja na fedha kutoka Misri akakamatwa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Cairo wakati si kweli.  
Alisema baadaye walidai ubalozi wa Misri hapa nchini utalipa hizo fedha, lakini ulipoulizwa ulikana na ndipo TFF ilipojitolea kuwaandikia Yanga SC hundi ya dola 35,000 na dola 10,000 kwa Stars TV ili mechi ionyeshwe.
“Sisi tulikubali kupokea hundi ya TFF mechi ionyeshwe, lakini Star TV wakagoma kupokea hundi ya TFF wakaondoka, sisi hatukuwafukuza kama wanavyodai hao jamaa, kimsingi hawa jamaa wametukosesha fedha dola 70,000.
“Kuna kampuni nyingine ya Misri ilijitokeza ikiwa tayari kutupatia dola 100,000 kununua haki za TV za hiyo mechi, lakini sisi tukaheshimu mkataba wetu na MGB, ila mwisho wa siku uungwana wetu umetuponza,”alisema Katabaro

 

No comments:

Post a Comment