Tuesday 4 March 2014

Tutatetea kwa nguvu uhuru wa habari-Mukajanga

 

Katibu wa Baraza la Habari Tanzania (MCT), Kajubi Mukajanga amesema uwepo wa wanahabari na wadau wa habari kwenye Bunge la Katiba kutasaidia kutetea kwa nguvu zake zote vipengele vinavyotoa haki ya uhuru wa habari kwenye Rasimu ya Katiba.
Mukajanga, ambaye pia ni mmoja wa wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba, aliliambia gazeti hili mwishoni mwa wiki kuwa kupendekezwa kwa uhuru huo ni jambo moja na kupitishwa kwa vifungu hivyo ni jambo jingine.
Kwa mujibu wa Rasimu ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano, Ibara ya 31 (1) inapendekeza haki ya kila mtu kuwa na uhuru wa kutafuta, kupata, kutumia na kusambaza habari na taarifa.
Pia Rasimu hiyo inatoa haki kwa mtu kuanzisha vyombo vya habari na njia nyingine za upashanaji wa habari bila kujali mipaka ya nchi na vitakuwa huru kupata, kutumia na kusambaza habari.
Kajubi, ambaye kitaaluma ni mwandishi wa habari, alisema jambo kubwa ambalo tayari ameshalifanya ni kuwatambua wadau wa habari ndani ya Bunge hilo, ambao atashirikiana nao katika kusukuma agenda hiyo.
“Mapendekezo yetu karibu yote tuliyoyatoa mbele ya Tume ya Jaji Warioba (Joseph) yameingizwa kwenye hii Rasimu. Jukumu letu sisi (wajumbe) sasa ni kushawishi ili yaweze kupitishwa bungeni,” alisema.
Kajubi pia alisema wadau wote wa habari, likiwemo Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) na waandishi wenyewe, wana wajibu mkubwa wa kushawishi kuhusu kupitishwa kwa ibara hizo.
Kwa mujibu wa rasimu hiyo, masuala mengine yaliyomo ni haki ya vyombo vya habari kuwa huru kusambaza taarifa kwa wananchi.
Pia kulinda utu, heshima na staha ya wananchi dhidi ya habari hizo.
Ibara ya 31(4) inaibana Serikali na taasisi zake, asasi za kiraia na watu binafsi kuwa na wajibu wa kikatiba wa kutoa habari kwa umma juu ya shughuli na utekelezaji wa shughuli zao.

 

No comments:

Post a Comment