Monday 31 March 2014

Kweli Serikali itadhibiti ada kubwa vyuoni?

Kwa muda mrefu wananchi wa kada mbalimbali wamekuwa wakilalamika kuhusu karo kubwa zinatozwa shuleni na katika vyuo vya elimu ya juu.
Kuna shule hapa nchini ambazo ada yake kwa mwaka inazidi kiwango kinachotozwa katika baadhi ya vyuo vikuu.
Hata hivyo, tatizo linatajwa kuwa kubwa zaidi kwenye vyuo vikuu. Kwa mfumo ulivyo nchini wanafunzi wanapoomba nafasi vyuoni, wanaweza kupangiwa chuo chohote.
Hali hii imekuwa ikiwaathiri wanafunzi wanaotoka katika familia masikini, kwa sababu wanajikuta wamepangiwa chuo kinachotoza karo kwa kiwango kikubwa.
Vyuo ni tofauti na shule kwa sababu mzazi ndiye anayeamua wapi ampeleke mwanawe kulingana na uwezo wa fedha alionao.
Inawezekana hili linalotokea katika taasisi za elimu ya juu ndilo lililoisukuma Serikali kuanzisha kile ilichokiita kama mfumo mpya wa upangaji ada kwa vyuo vikuu.
Akizindua mfumo huo hivi karibuni, Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk. Shukuru Kawambwa alisema utasaidia kudhibiti viwango vya ada vinavyotozwa kwa wanafunzi.
Alisema Serikali imeanzisha mfumo huo utakaoanza kutumika mwaka huu katika vyuo vyote, kwa lengo la kudhibiti ada kulingana na fani zinazotolewa.
Kwa mujibu wa Dk. Kawambwa, mfumo huu ambao baadaye utaendelea hadi shule za sekondari na msingi, umepatikana kupitia kikosi kazi cha wataalamu ambacho pamoja na majukumu mengine kilipewa kazi ya kutathmini gharama.
Dk. Kawambwa alisema moja ya faida ya utaratibu huo mpya ni kudhibiti taasisi zinazotoza ada kubwa kwa sababu za binafsi ikiwamo biashara.
Itakumbukwa pia kuwa, Aprili 2013 akifungua mkutano mkuu maalumu wa Chama cha Wamiliki na Mameneja wa Shule na Vyuo Visivyokuwa vya Serikali (Tamongsco) uliofanyika mkoani Mbeya, Rais Jakaya Kikwete alisema: “Elimu ni huduma muhimu na haki kwa mtoto kwa hiyo si vyema kugeuzwa kuwa biashara ya faida kubwa.’’
Pamoja na nia njema ya Serikali, nina shaka na utekelezaji wa mfumo huu. Kila ninapoutazama kwa jicho la ndani sioni zaidi ya ugumu katika kuutekeleza.

 

No comments:

Post a Comment