Monday 31 March 2014

Wafanyabiashara Mwika walalamikia ushuru magari

Moshi. Wafanyabiashara wa mazao ya ndizi na maparachichi katika Soko la Mwika lililopo Wilaya ya Moshi mkoani Kilimanjaro wamelalamikia ongezeko la ushuru wa magari makubwa katika soko hilo.
Hali hiyo imesababisha wenye magari kuhamisha magari yao na kuyapeleka Soko la Mamsera wilayani Rombo na kuwaacha wananchi wa Mwika wakishindwa kuuza bidhaa zao.
Wafanyabiashara hao walikuwa wakiuza bidhaa hizo kwa wafanyabiashara wakubwa wa jijini Dar es Salaam, Kenya na mikoa ya jirani, lakini kwa sasa bidhaa hizo haziuziki baada ya wafanyabiashara wakubwa kukimbia ushuru ulioongezwa na wakala kutoka Sh 40,000 hadi Sh 60,000
Mbunge wa Jimbo la Vunjo, Dk. Agustino Mrema alikiri kupokea malalamiko hayo na tayari amewasiliana na mkurugenzi wa halmashauri hiyo kufuatilia malalamiko.
Mrema alimuomba mkurugenzi wa Manispaa ya Moshi kuingilia kati na kukaa na wakala pamoja na wafanyabiashara, ili kutoharibu biashara katika soko la kimataifa ambalo linawaleta wafanyabiashara kutoka ndani na nje ya nchi.
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Manispaa ya Moshi, Fulgence Mponji hakuweza kupatikana kuzungumzia malalamiko hayo. baada ya simu yake ya mkononi kutopatikana.

 

No comments:

Post a Comment