Monday 31 March 2014

Ukawa waanza mapambano nje ya Bunge

Mjumbe wa Bunge la Katiba wa kundi la Umoja wa Kutetea Katiba ya Wananchi (Ukawa), Ismail Jussa akionyesha moja ya nukuu za kitabu cha Profesa Issa Shivji wakati wa mkutano na waandishi Dodoma jana. Kushoto ni mjumbe mwenzake, Tundu Lissu. Picha na Salima Shao

Dar /Dodoma/Mwanza. Ni dhahiri kwamba mjadala wa msomi wa Sheria, Profesa Issa Shivji umewavuruga wanasiasa waumini wa serikali mbili ambao baadhi yao jana walimshukia wakidai kuwa “mzee huyu ni ndumila kuwili na kigeugeu.”
Shivji juzi alitoa mjadala kuhusu muundo wa Muungano na kuishutumu Tume ya Mabadiliko ya Katiba iliyopendekeza serikali tatu, kuwa ilipotosha maoni ya wananchi. Alipotakiwa kuzungumzia madai dhidi yake, Profesa Shivji alisema: “Nyie ni waandishi wa habari someni, angalieni wapi mimi nilisema Serikali tatu, wanaosema ninatumiwa na CCM hayo ni maoni yao siwakatazi kuzungumza wanachofikiria.”
Jana Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) katika kampeni yake nje ya Bunge la Katiba, ulimtaka Profesa Shivji kuwaomba radhi wananchi kwa kile wanachodai kwamba amekuwa kigeugeu kwenye maandishi na matamshi yake kuhusu muundo wa Muungano.
Katika mkutano wake wa kuelimisha wananchi kuhusu Katiba Mpya mjini Mwanza uliojaa polisi kila kona, Katibu Mkuu wa Chadema, Dk. Willibrod Slaa alisema wanamshangaa Profesa Shivji kwa mawazo yake yasiyoeleweka kuhusu muundo wa Muungano.
“Kwa kweli tunaamini watu ambao ni wasomi kama Profesa Shivji wanaweza kuwasaidia wananchi kupata katiba nzuri, lakini anachokifanya sasa ni siasa, jambo ambalo siyo jema,” alisema Dk. Slaa na kuongeza:
“Ukawa tunamtaka awaombe radhi wananchi, kwani amewadhalilisha kwa kuwa kigeugeu. Mara ya kwanza tunakumbuka alikuwa muumini wa Serikali tatu leo anageuka na kuanza kuhubiri serikali mbili, huu ni upuuzi kwa msomi kama yeye kufanya hivyo.”
Katibu Mkuu wa NCCR-Mageuzi, Mosena Nyambabe alisema CCM wanaogopa Rasimu ya Katiba kwa sababu wamezoea uchakachuaji.
Naye Kaimu Katibu Mkuu wa CUF, Abdulkarim Kambaya alisema Rais Kikwete amewachezea akili wananchi, kwani awali alikuwa anaonyesha yupo upande wao lakini kupitia hotuba yake bungeni amewakana na kuibeba CCM.
Lissu, Jussa nao wanena
Pia baadhi ya wajumbe wa Bunge la Katiba wanaounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) jana walimshambulia kwa maneno Profesa Isa Shivji kuwa ni ‘ndumilakuwili’.
Kwa nyakati tofauti, wajumbe Tundu Lissu na Ismail Jussa walisema kuwa Profesa Shivji “alibebwa na CCM na kulishwa maneno kwa masilahi ambayo hayajulikani.”
Akizungumzia hotuba hiyo, Jussa aliyeweka wazi masilahi yake kuwa ni mwanafunzi wa Profesa Shivji, alisema msomi huyo aliyekuwa tegemeo la wanyonge, alifanya upotoshaji mkubwa ambao umetoa vitisho kwa wananchi.

 

No comments:

Post a Comment