Monday 31 March 2014

Sitta ampa barua Mtikila aende kwa JK

Mwenyekiti wa Bunge la Katiba,Samuel Sitta.

Dodoma. Ombi la Mjumbe wa Bunge la Katiba, Mchungaji Christopher la kutaka Bunge hilo livunjwe, limekuwa zito kwa Mwenyekiti Samuel Sitta.
Kutokana na ugumu huo, Sitta amelazimika kumpatia barua Mtikila ili awasilishe hoja yake kwa Rais Jakaya Kikwete, ambaye kisheria ana mamlaka hayo ya kuvunja Bunge la Katiba, ambalo limekuwa likionekana kwenda mrama.
Mtikila, ambaye ni mwenyekiti wa Chama cha Kidemokrasia na mjumbe wa Bunge la Katiba aliwasilisha barua yenye hoja binafsi akitaka bunge hilo livunjwe na wajumbe warejee makwao kwa madai kuwa chombo hicho cha kutunga Katiba mpya hakijali maslahi ya umma na uongozi umekuwa haumtendei haki.
Majibu ya barua hiyo yalikuwa hivi: “Nimeagizwa na Mwenyekiti wa Bunge Maalumu nikujulishe kwamba Bunge Maalumu halina uwezo wala mamlaka ya kujitangaza kwamba ni haramu na hivyo livunjwe ; na kwamba hoja hiyo haistahili kuwa hoja ya Bunge Maalumu,” inasomeka barua hiyo iliyoandikwa na katibu wa Bunge hilo, Yahya Khamis Hamad.
Akizungumza na Mwananchi jana, Sitta alikiri kumpatia barua hiyo Mtikila ili aende kwa Rais Kikwete kwa sababu hoja yake kutaka kuvunjwa Bunge haiwezi kusikilizwa na chombo hicho kwa kuwa mwenye madaraka ya kuvunja Bunge ni Rais pekee.
“Ni kweli ametuletea hoja ya kuvunja Bunge. Ameandika mambo mengi, akitumia lugha ya uchochezi, kama kudai kwamba ‘Tanganyika imekuwa koloni la Zanzibar kwa muda mrefu’, lugha ya namna hii hatuwezi kuikubali,” alisema Sitta.
Sitta alisema siyo kila kitu ambacho mjumbe anasema, ni lazima kifuatwe katika mchakato huu wa kuandika Katiba Mpya.
“Mtu akija anasema anataka Bunge livunjwe amfuate aliyetuteua, siyo sisi wenyewe kujivunja,” alisema Sitta.
Alisema hoja ya Mtikila, ambaye alitishia kufungua kesi ya kuzuia Bunge la Katiba kufanya kazi, ya kutaka Bunge kuvunjwa imekwenda kinyume kabisa na taratibu za Bunge.
“Hoja hii imekwenda nyuzi 180 kwa sababu aliyetuteua alitaka sisi tutunge katiba kutokana na rasimu, ili sisi tupeleke kwa wananchi rasimu iliyopendekezwa,” alisema.
Mchungaji Mtikila alikiri kupokea barua kutoka Ofisi ya Bunge ikimweleza jambo moja; apeleke hoja yake kwa Rais Kikwete aliyeteua Bunge la Katiba.
Hata hivyo, alisema hakusudii kwenda kumuona Rais Kikwete baada ya kushauriwa kupitia barua ya Bunge kutokana na kutoa hoja ya kutaka kuvunjwa kwa bunge hilo.

No comments:

Post a Comment