Monday 31 March 2014

Mvua zaleta maafa makubwa Dar, mikoani

Mkazi wa Kijiji cha Bulembo mkoani Kagera, Godena Joseph akitafakari baada ya shamba lake la migomba kuharibiwa na mvua iliyoambatana na upepo. Picha na Issa Ibrahim.  

ar/Pwani/Kagera. Mvua zilizonyesha maeneo mbalimbali nchini tangu wiki iliyopita, zimesababisha maafa, uharibifu wa mali, miundombinu na kuacha zaidi ya familia 150 bila makazi.
Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili, umebaini kuwa athari za kifamilia zimeukumba zaidi Mkoa wa Kagera ambako familia zaidi ya 125 zinahitaji msaada baada ya nyumba zao kuezuliwa paa na mashamba ya migomba kuharibiwa.
Ingawa maeneo mengi ya nchi yameathirika, hali inaonekana ni ya kiwango cha juu zaidi katika mikoa ya Dar es Salaam, Bukoba, Lindi na Mtwara.
Jijini Dar es Salaam, maeneo kadhaa yamejaa maji na hata kusababisha watu kuyakimbia makazi yao kama vile Jangwani, Bonde la Mto Msimbazi na Mbweni ambako Serikali ilipima viwanja na kuvigawa kwa wananchi.
Mkoani Kagera, maeneo yaliyoathirika zaidi ni ya vijiji vya Bulembo, Kata ya Kamachumu wilayani Muleba.
Mbunge wa Muleba Kaskazini, Charles Mwijage alisema: “Hali siyo nzuri na timu ya watalaamu ipo eneo la tukio ili kufanya tathmini zaidi kuhusu kadhia hiyo.
“Watu wa Msalaba Mwekundu wanajaribu kurejesha paa upya katika baadhi ya nyumba zilizoezuliwa.”
Mkazi wa Kijiji cha Bulembo, Richard Kichabeba alisema familia zilizokumbwa na tatizo la nyumba zao kuezuliwa paa, zinaishi nje na mbaya zaidi nyumba zinazidi kuporomoka kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha.
“Hakuna muhogo wala mgomba. Mawe na upepo vimevuruga kila kitu,” alisema mkazi huyo na kuongeza kuwa mbaya zaidi hata hizo paa zao hazijulikani zimeangukia wapi.
Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo, Ahmed Kipozi alisema kuwa uongozi wa wilaya hiyo umelazimika kuifunga kwa muda usiojulikana Barabara ya Msata – Bagamoyo baada ya maji kuifunika.
Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Kibaha, Halima Kihemba alisema kuwa hivi sasa Kata mbili za Ruvu na Kwala hazifikiki baada ya madaraja kubomoka.
Alisema kuwa madaraja mawili ya Mto Ndwati na Msua yamefurika maji hali iliyosababisha mafuriko makubwa, hivyo aliwataka wakazi wa vijiji hivyo kuchukua tahadhari.

 

No comments:

Post a Comment