Monday 31 March 2014

Magaidi waua watu 6 Kenya 

Watu sita wameuawa na wengine 25 kujeruhiwa vibaya katika shambulizi la kigaidi katika eneo la California mtaa wa Eastleigh, viungani mwa mji wa Nairobi.

Waathiriwa wa shambulizi wakipelekwa hospitalini 

Kamanda wa Polisi mjini Nairobi Benson Kibue amesema kuwa milipuko miwili ilitokea wakati magaidi waliporusha vilipuzi katika mikahawa miwili midogo.
Mlipuko wa tatu ulitokea katika kituo cha mabasi ya uchukuzi kilichoko karibu na zahanati za afya ya mama na mtoto.
Miongoni mwa waliojeruhiwa walikuwa ni wanawake waliokuwa wanauza mboga na bidhaa zingine za rejareja.
Kwa mujibu wa polisi wale waliouawa walikuwa wamekwama ndani ya mkahawa huo baada ya mlango kufungwa kutoka nje na washambulizi waliorusha bomu ndani .
Waathiriwa walikuwa wameenda kununua chakula cha jioni.
Idadi kubwa ya wakimbizi wa kisomali wanaishi katika mtaa wa Eastleigh.
Inaarifiwa washambuliaji walitumia maguruneti au mabomu ya kutengezwa nyumbani kufanya mashambulizi hayo
Mashambulizi haya yanawadia siku moja tu baada ya mtu anayeshukiwa kuwa gaidi kufa kilipuzi alichokuwa akikiunganisha kilipolipuka .
Isitoshe wakenya bado wanaomboleza vifo vya waumini 6 waliouawa katika kanisa moja mjini likoni Mombasa majuma mawili yaliyopita.
Mtaa wa Eastleigh unafahamika kama ''Mogadishu ndogo'' kutokana na idadi kubwa ya wasomali wanoishi hapo wengi wakiwa ni wakimbizi.
Mtaa huu ambao ni kitovu cha biashara umepigwa darubini na serikali ya Kenya haswa baada ya visa vingi vya ugaidi kuhusishwa na kundi la wapiganaji wa kiisalmu la Al Shaabab ambao wamepinga vikali kuweko kwa majeshi ya Kenya nchini Somalia kama sehemu ya AMISOM.

No comments:

Post a Comment