Monday 31 March 2014

Sasa tuseme ajali za mabasi zimetosha ajali hizi basi

Pamoja na ubora huo, pia mafunzo ya madereva yaangaliwe upya ili kabla ya mtu kupewa leseni awe ameiva, leseni pia tunashauri zidhibitiwe.

Kwa mara nyingine, nchi yetu imepata janga jingine kubwa baada ya ajali mbili kutokea katika mikoa ya Pwani na Kilimanjaro mwishoni mwa wiki iliyopita na kusababisha vifo kwa watu zaidi ya 30.
Ajali ya kwanza ilitokea Hedaru wilayani Same, Kilimanjaro ambayo imesababisha vifo vya waombolezaji 12. Nyingine ni ile iliyotokea Rufiji mkoani Pwani ambayo imeua watu 22 na wengine kadhaa kujeruhiwa.
Tunachukua nafasi hii kipekee kuwapa pole majeruhi wa ajali hizi, tukiwaombea ili wapate nafuu haraka na kuendelea na majukumu yao.
Aidha, tunawapa pole waliofiwa na ndugu, jamaa na marafiki zao katika ajali hizi, hasa kipindi hiki kigumu cha majonzi. Hakuna shaka, ajali hizi ni mfululizo wa matukio ya kusikitisha yanayoendelea kutokea katika barabara nyingi nchini.
Ajali hizi hazitokani na uzembe wa madereva pekee, bali matumizi duni ya barabara zetu ikiwamo nyakati wa mvua za masika au hata kiangazi kutokana na vumbi. Tunashauri kila mtumiaji wa barabara awe makini, atimize wajibu wake ipasavyo.
Tukitumia mfano wa ajali za Same na Rufiji, jambo linalofanana ni magari yaliyohusika katika ajali hizo kugongwa na mengine kwa nyuma. Haya yametokea wakati kuna madai kuwa magari yamekuwa yakiachwa barabarani kwa muda mrefu yakiharibika bila kuondolewa.
Hii, tunasema inaweza kuwa sababu ya magari kugongana na kuuua abiria. Huu, bila shaka ni ushahidi wa jinsi ambavyo madereva, baadhi yao wasivyokuwa makini katika kuendesha vyombo vya moto. Tunashauri, wasimamizi wa uchunguzi wa magari, usalama wake wawe makini ili magari yanayoruhusiwa kuingia barabarani, kubeba abiria yawe kwenye ubora na viwango vinavyostahili.
Pamoja na ubora huo, pia mafunzo ya madereva yaangaliwe upya ili kabla ya mtu kupewa leseni awe ameiva, leseni pia tunashauri zidhibitiwe.
Ni wazi, kuruhusu magari yakiwamo malori madogo maarufu kama kirikuu kubeba abiria jioni au usiku ni mambo ambayo hayakubaliki na ni hatari. Hali hii inatokea katika maeneo mengi nchini ikiwamo Dar es Salaam, ambako askari wapo barabarani mchana kutwa.
Tunasema, udhaifu huu umekuwa sababu ya vifo, nasi kama jamii tunabaki kimya.
Tunashangazwa, kwa mfano, na ruhusa nyingine kwa magari madogo ya mizigo (pick-up), ya familia kama Toyota Noah na mengi yakiwa chakavu kuruhusiwa kubeba abiria.
Tunasema hivyo kwa muwa ndivyo ilivyotokea Same. Ni jambo linalosikitisha kwa kuachwa liendelee huku askari wa usalama barabarani wakishuhudia kana kwamba ni jambo la kawaida. Ruhusa hizi kwa malori madogo kubeba abiria ni jambo linalofanyika Dar es Salaam, mahali ambako kuna askari wengi wa usalama barabarani, lakini hakuna hatua zinazochukuliwa. Ukimya huu katika roho za watu ni wa nini?

 

No comments:

Post a Comment